Mshindi wa mechi ya leo atafuzu moja kwa moja hadi fainali iliyoratibiwa kuchezwa tarehe 8 Disemba mjini Kisumu. Picha CECAFA

Mashindano ya CECAFA ya soka la ukanda kwa wavulana, CECAFA U18 yanayoendelea Kenya, yameingia nusu fainali.

Timu ya taifa ya soka ya wavulana ya Kenya itachuana na Tanzania uwanjani Jomo Kenyatta mjini Kisumu nchini Kenya, katika kile kinachotarajiwa kuwa mchuano wa hali ya juu kati ya pande hizo mbili.

Kenya ilitinga nusu fainali moja kwa moja baada ya kumaliza viongozi wa Kundi A kwa kushinda mechi zake zote 100%.

Tanzania ilifuzu nusu fainali kwa kigezo cha kuwa na nidhamu ya hali ya juu baada ya kumaliza sawa kwenye idadi ya alama (4) na pia kufunga idadi sawa ya mabao na Zanzibar.

Wenyeji Kenya wanategemea motisha ya mashabiki wa nyumbani watakapochuana na Tanzania huku Uganda ikikabiliana na Rwanda kwenye mechi hizo za kufana za nusu fainali.

Hata hivyo, rais wa Shirikisho la Soka la Tanzania TFF, Wallace Karia, amefika mjini Kisumu kuipa motisha timu ya Taifa ya Wavulana ya Tanzania U18.

Timu hiyo ya Tanzania inaongozwa na kocha Habibu Kondo huku Kenya ikiongozwa na Salim Babu.

Mshindi wa mechi ya leo atafuzu moja kwa moja hadi fainali iliyoratibiwa kuchezwa tarehe 8 Desemba mjini Kisumu, kuhitimisha kile kilichokuwa Kombe kla kufana kilichovutia jumla ya timu nane.

Nyota wa Kenya na mfungaji bora wa Kombe hilo, Aldrine Kipchirchir Kibet anatarajiwa kuwa tegemeo la Kenya kwa mara nyingine katika mechi hiyo

TRT Afrika