Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Kenya Musalia Mudavadi anasema kuwa nchi yake haiingilii maswala ya ndani ya DR-Congo. / Picha: AFP

Kenya imekanusha kuwa inaunga mkono muungano mpya wa waasi wa DR-Congo ambao ulianzisha shughuli zake Nairobi, mji mkuu wa Kenya, siku ya Ijumaa.

Corneille Nangaa, mkuu wa zamani wa baraza la uchaguzi la DR-Congo, alitangaza kuwa makundi tisa ya waasi wa Kongo, wakiwemo M23, wameungana na kuunda Muungano wa Mto Congo (AFC) kwa lengo la kurejesha amani.

Msemaji wa serikali ya DR-Congo Patrick Muyaya alilaani Kenya kwa kuandaa "muungano haribifu" na kuonya kuwa "utaathiri uhusiano wa kidiplomasia."

Baada ya tangazo la kuundwa kwa AFC, DR-Congo ilimwita balozi wake nchini Kenya, John Nyakeru Kalunga, kwa "mashauriano" siku ya Jumamosi.

'Inajitenga kabisa'

'Inajitenga kabisa'Kenya sasa inasema "inajitenga na matamshi au shughuli zozote zinazoweza kudhuru amani na usalama wa taifa rafiki la DRC."

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Kenya Musalia Mudavadi alisema katika taarifa Jumapili kwamba serikali ya Kenya "imeanza uchunguzi ili kubaini ni nani waliounda tamko la (muungano mpya wa waasi) na ni kwa kiwango gani matamshi yao yanatoka nje ya hotuba inayolindwa na katiba."

"Kenya inathibitisha zaidi kutojihusisha na masuala ya ndani ya DRC na inajitolea kuendelea kuunga mkono amani, usalama na uimarishaji wa kidemokrasia nchini," Mudavadi alisema.

Serikali ya Kenya iliongeza kuwa "nchi ya kidemokrasia ambapo uhuru wa vyombo vya habari umeidhinishwa, raia na wasio raia wanaweza kushirikisha vyombo vya habari vya Kenya bila kurejelea serikali."

DR-Congo, haswa eneo la mashariki mwa nchi, limekuwa likikabiliwa na tatizo la ukosefu wa usalama, huku zaidi ya makundi 100 ya wapiganaji yakiendesha harakati zake katika eneo hilo lenye machafuko.

TRT Afrika