Ukatili wa Israeli dhidi ya Wapalestina kwa zaidi ya miezi 7 unazidi kutatiza wakazi wa Gaza. /Picha: AA

Uturuki inapongeza azimio lililopitishwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la kusitishwa kwa mapigano huko Gaza, imesema Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki, na kuiita "hatua muhimu."

"Tunazingatia azimio nambari 2735 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lililopitishwa tarehe 10 Juni, ambalo linalenga kuleta usitishaji vita huko Gaza, kama hatua muhimu ya kukomesha mauaji," taarifa ya wizara hiyo ilieleza Jumanne.

"Tunakaribisha mtazamo mzuri wa Hamas katika mpango wa kusitisha mapigano," iliongeza.

Kauli hiyo imekuja baada ya Baraza la Usalama siku ya Jumatatu kupitisha azimio lililoandaliwa na Marekani linalounga mkono pendekezo lililotolewa na Rais wa Marekani Joe Biden la kusitisha mapigano Gaza. Urusi ilijizuia kupiga kura hiyo, huku wajumbe 14 waliosalia wakipiga kura ya ndio.

"Ni muhimu kwamba Israeli itangaze dhamira yake ya utekelezaji wa usitishaji vita wa kudumu na kutekeleza kikamilifu vipengele vyote vya azimio hilo," wizara hiyo ilisema.

Uturuki itaendelea kuchangia katika hatua zitakazohakikisha kusitishwa kwa vita, kuondolewa kwa Israeli kutoka eneo la Gaza lote, kuachiliwa kwa mateka na wafungwa kutoka pande zote mbili, kurejea kwa Wapalestina waliokimbia makazi yao huko Gaza, uingizaji wa kutosha wa misaada ya kibinadamu na kujengwa upya kwa Gaza, wizara hiyo iliongeza.

TRT World