Na Coletta Wanjohi , Addis Ababa, Ethiopia
Waziri wa Mambo ya Nje wa Djibouti Mahmoud Youssouf sasa anachukua nafasi ya uongozi wa mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika.
Alipata theluthi mbili ya kura zinazohitajika baada ya wakuu wa nchi 33 kati ya 49 kumpigia kura wakati wa uchaguzi na viongozi wa Afrika katika mkutano wao wa kilele wa kila mwaka mjini Addis Ababa Ethiopia 15 Februari 2025.
Youssouf anachukua nafasi hiyo kutoka kwa Moussa Faki Mahamat wa Chad aliyehudumua kwa awamu mbili za miaka minane.

Kenya ambayo mgombea wake, waziri mkuu wa zamani Raila Odinga alikuwa mshindani mkuu wa Youssouf ilikubali kushindwa.
“Uchaguzi huu haukuwa wa watu binafsi au mataifa; ilihusu mustakabali wa Afrika. Mustakabali huo unasalia kuwa angavu na, kwa pamoja, tutaendelea kufanya kazi kwa ajili ya Afrika iliyoungana, yenye ustawi na ushawishi katika ulimwengu mzima,” Rais wa Kenya William Ruto alisema alipokuwa akiipongeza Djibouti kwa ushindi wake kupitia akaunti yake ya X.
Madagascar ambayo ilikuwa na kura za chini sana na kulazimika kujiondoa katika awamu za kwanza za uchaguzi pia ilikubali kushindwa.
"Nakubali kwa unyenyekevu, matokeo ya duru hii ya 3 ya uchaguzi wa urais wa AUC ambapo ugombea wangu uliondolewa kutokana na kura zisizotosha," Richard Randriamandrato mgombeaji wa nchi hiyo alisema kwenye akaunti yake ya X.
Ni nini kilichangia ushindi wa Djibouti?
Katika uchaguzi wa Tume ya Umoja wa Afrika mambo kadhaa yanaathiri upigaji kura.
Kwanza limegawanyika kati ya nchi zinazotumia Kiingereza kama lugha rasmi na zile zinazozungumza kifaransa.
Kuna nchi 26 zinazozungumza Kifaransa barani Afrika huku 27 zikijiorodhesha kuwa zinazungumza Kiingereza
Nchi zingine zina Kiingereza na Kifaransa, wakati zingine 6 zinazungumza Kireno.
Katika hali hii mgombea wa Djibouti Youssouf ambaye nchi yake ni kati ya zile za kuongea kifaransa, hiyo ni kati ya kivutio kikubwa cha kura kutoka nchi zingine zinazozungumza lugha hiyo moja kwa moja.
"Ujuzi mahiri wa Youssouf wa kidiplomasia, mawasiliano, na lugha nyingi uliimarisha zaidi kufaa kwake kwa jukumu hilo," Nuur Mohamud Sheekh, mchambuzi na msemaji wa zamani wa Mamlaka ya Maendeleo ya Kiserikali, anaiambia TRT Afrika.
Pili ni kipengele cha dini. Kulingana na mifumo ya awali ya upigaji kura ya kiti cha juu cha Tume ya Umoja wa Afrika, ni rahisi kuvutia kura kwa nchi zinazotambua Uislamu au Ukristo kama dini zao maalum- kulingana na dini ambayo nchi husika inatambua.
Lakini wataalam wanasema mienendo ya kijiografia na kisiasa ni suala kubwa.
Kwa mfano, ukaribu wa nchi inayotafuta kura kwa zingine, uhusiano wa kisiasa, kijamii na kiuchumi ambao nchi hiyo ina nao na wengine unaweza kushawishi kura ya kuwapendelea.
"Sifa ya muda mrefu ya Djibouti kama nguzo ya utulivu na jukumu lake la kimkakati katika diplomasia ya kikanda, ikiwa ni pamoja na kama mwenyeji wa makao makuu ya Mamlaka ya Maendeleo ya Kiserikali (IGAD), bila shaka ilichangia matokeo," Nuur Sheek anaiambia TRT Afrika.
Wagombea hao watatu, kutoka Kenya, Djibouti na Madagascar, walieleza maono yao wakati wa mdahalo wa hadhara ulioandaliwa na Tume ya Umoja wa Afrika tarehe 13 Desemba 2024.
Walirudia tena kuelezea tena mipango yao mbele ya marais kabla ya kura kupigwa.
"Maono yenye mvuto ya mgombea kwa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), iliyofafanuliwa ipasavyo katika mazungumzo yake ya umma na wakati wa mjadala wa AUC, ilikuwa jambo muhimu katika kupata kuungwa mkono kwa mapana," sheekh anaongeza.
Uzoefu katika masuala ya bara mara nyingi ni faida kwa mgombea. Mgombea wa Djibouti ni waziri wa mambo ya nje wa nchi hiyo na anawakilisha nchi katika bara na kimataifa
Hiyo ina maana kwamba tayari anafahamu vyema kazi ya Umoja wa Afrika. Mgombea wa Djibouti alikuwa na umri wa miaka 60 huku wa karibu wake Raila Odinga akiwa na umri wa miaka 80.
"Kama mmoja wa mawaziri wa mambo ya nje waliokaa muda mrefu zaidi barani Afrika, utaalam wake wa kina ulikubaliwa, lakini mazingatio ya vizazi pia yalichukua jukumu - kuakisi matarajio ya raia wa bara la Afrika kwa kiongozi mchanga na mahiri ili kuendeleza ajenda ya Muungano,"
Je, ni changamoto zipi kwa mwenyekiti mpya wa AUC?
Jukumu kuu ya mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika ni kuhakikisha utekelezaji wa uamuzi uliotolewa na wakuu wa nchi za Afrika ambao unahusu utekelezaji wa ajenda ya Afrika ya 2063.
Youssouf anakuja kwenye uongozi wakati bara linapambana na changamoto za amani na Usalama.

"Kuongezeka kwa ugaidi na itikadi kali za itikadi kali na kuendelea kwa vita haribifu nchini Sudan, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, mgawanyiko wa kisiasa nchini Libya ... mvutano wa kila aina katika eneo la Sahel katika bonde la Ziwa Chad, Ghuba ya Guinea ya Msumbiji katika pembe ya Afrika na Ukanda wa Maziwa Makuu ni mizozo ya Afrika," Moussa Faki Mahamat , mwenyekiti wa Tume ya AU aliyeondoka ameelezea.
Mwenyekiti mpya pia ana jukumu la kuhakikisha kuwa bara hilo linakuwa dhabiti katika kutekeleza matarajio ya kituo cha afya cha Afrika, Afrika CDC, mpango wa kuhakikisha kuwa taasisi hilo ina vifaa vya kutosha na kujitosheleza kifedha kukabiliana na changamoto za kiafya.
Youssouf pia anachukua uongozi wakati Umoja wa Afrika unatafuta ufadhili bora wa ndani kwa ajili ya shughuli zake, kufanya kampeni ya kutaka madeni ya kimataifa kufutwa pamoja na kutafuta kutekeleza Shirika la Kibinadamu la Afrika( African Humanitarian Agency.
Haya yote na mengine mengi ni majukumu yanayomngoja mwenyekiti mpya wa Tume ya Umoja wa Afrika, Mahmoud Youssouf.