Paul Mackenzie na mkewe wako rumande kwa madai ya kuwaelekeza wafuasi wao kufa njaa. Picha: Reuters

Mshukiwa mmoja aliyehusishwa na kikundi cha njaa nchini Kenya amefariki.

Joseph Juma Buyuka, ambaye alikuwa kizuizini katika gereza la Malindi katika Kaunti ya Kilifi, anaripotiwa kufariki wakati akipokea matibabu hospitalini.

"Tunashuku alifariki kwa sababu ya matatizo yaliyotokana na mgomo wa njaa. Tunasubiri uchunguzi wa maiti ufichue sababu halisi ya kifo chake," Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali Jami Yamina aliiambia mahakama katika pwani ya Kenya.

Washukiwa wengine wawili, Evans Sirya na Frederick Karimi, wamekimbizwa hospitalini baada ya kupata matatizo yanayohusiana na njaa, alisema Yamina.

Wawili hao, pamoja na Buyuka, walikuwa wameshikiliwa wakati mamlaka zinafanya uchunguzi kuhusu vifo vya zaidi ya watu 330, ambao wanadaiwa kuwa sehemu ya kikundi kinachoongozwa na mhubiri Paul Mackenzie.

Madai ya mauaji ya kimbari

Zaidi ya watu 35, ikiwa ni pamoja na Mackenzie na mke wake, wamekamatwa wakati serikali inachunguza madai ya mauaji ya kimbari.

Mwendesha mashtaka aliomba mahakama kusogeza mbele kusomewa mashtaka ya Sirya na Karimi hadi watakapotolewa hospitalini.

Inadaiwa kuwa Mackenzie aliwashawishi wafuasi wake kwamba kufunga sana kingewapeleka moja kwa moja kukutana na Yesu "katika maisha ya baadaye."

Vifo vilidaiwa kufuata mpangilio maalum: kwanza watoto, kisha wanawake, watu ambao hawajaolewa, waliokuwa wameolewa na hatimaye Mackenzie na familia yake.

Miili ya mamia ya watu imechimbwa kutoka makaburi madogo katika msitu wa Shakahola, eneo kubwa katika mji wa Malindi kusini mwa Kenya.

TRT Afrika