George Weah aongoza Uchaguzi wa Urais Liberia. Picha: Getty

Rais wa Liberia George Weah ndiye anaongoza matokeo ya awali ya uchaguzi wa Urais wa Liberia huku akiwa na uongozi mwembamba dhidi ya aliyekuwa makamu wa rais wa zamani Joseph Boakai.

Haya yanajiri huku tume ya uchaguzi ya Liberia (NEC) ikiendelea kutangaza matokeo ya awali ya uchaguzi ulioandaliwa nchini humo tarehe 10 Oktoba.

Kulingana na matokeo ya awali kutoka tume ya kitaifa ya uchaguzi nchini Liberia, takriban 50% ya kura ya zaidi ya watu milioni 2.4 kutoka vituo 5,890 vya kupigia kura, George Weah amepata asilimia 44.58 ikiwa sawa na kura 415,895 naye Boakai amepata asilimia 43.1 ambayo ni sawa na kura 402,137.

Weah, mwenye umri wa miaka 57, mwanasoka mstaafu aliyegeuka mwanasiasa, anasaka kudumisha kiti hicho kwa kuchaguliwa tena huku akishindana na jumla ya wagombea 19, ambao wanawania kiti hicho katika taifa hilo la Afrika magharibi.

Joseph Boakai, ambaye ni makamu wa rais wa zamani wa Liberia mwenye umri wa miaka 78, anashindania kiti hicho cha urais kwa mara ya pili baada ya kupoteza dhidi ya Weah katika raundi ya pili ya uchaguzi wa 2017.

Rais Weah ambaye alipiga kura siku ya jumanne, amewataka raia wa Liberia kudumisha amani.

Ili kutangazwa mshindi wa uchaguzi, mgombea anahitaji kupata zaidi ya asilimia 50 ya jumla ya kura zilizopigwa.

Tume ya uchaguzi Liberia inatarajiwa kutangaza matokeo rasmi tarehe 25 Oktoba.

TRT Afrika na mashirika ya habari