Katibu Mkuu wa EAC Veronica Mueni Nduva akila kiapo, Juni 7, 2024./Picha: EAC

Na Edward Qorro

TRT Afrika, Istanbul, Uturuki

Katibu Mkuu mpya wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Veronica Mueni Nduva ameazimia kukuza mtangamano na kuchochea maendeleo ya raia wa Afrika Mashariki.

Akizungumza mara baada ya kula kiapo wakati wa mkutano wa dharura wa 23 wa Wakuu wa Nchi za EAC uliofanyika kwenye Ikulu ya Juba, huko Sudan Kusini, Nduva alibainisha vipaumbele vyake kuwa ni pamoja na kuimarisha mtangamano wa kiuchumi wenye kuchochea ubunifu, ujasiriamali, kutengeneza ajira na hatimaye kukuza amani na usalama wa kikanda.

“Waheshimiwa Marais, katika kukuza amani na usalama katika kanda yetu, ni vyema kuwa na Jumuiya iliyosalama yenye kukuza ustawi wetu,” alisema Katibu Mkuu huyo.

Pia, maendeleo ya miundombinu yatatawala ajenda ya Katibu Mkuu huyo akisisitiza kuwa ni muhimu kwa sekta hiyo kukua kupitia ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi.

"Ili kuimarisha ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi, tutaendelea kushughulikia changamoto kubwa za mabadiliko ya hali ya hewa kwa pamoja kama kanda. Hii ni pamoja na kukuza nishati ya kijani, kilimo endelevu, juhudi za uhifadhi na uhamasishaji wa rasilimali kama kambi,” aliongeza.

Katibu Mkuu wa EAC, Veronica Mueni Nduva akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya hiyo, Rais Salva Kiir Mayardit wa Sudan Kusini./Picha: EAC

Mnamo Aprili 15, 2024, Serikali ya Kenya ilipitisha jina la Veronica Mueni Nduva kama mbadala wa Caroline Mwende Mueke ambaye hakuwah kuapishwa.

Kwa mujibu wa kifungu hicho cha sheria, Katibu Mkuu wa EAC, anapaswa kuhudumu kwa kipindi cha miaka 5.

Kulingana na itifaki ya kuanzisha EAC, Rais wa nchi husika anaweza kupendekeza jina kwa nafasi ya Katibu Mkuu, kabla ya kuidhinishwa na Mkutano wa Wakuu wa nchi za Afrika Mashariki.

Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ni muundo wa kisiasa unaohusisha nchi nane, na makao makuu yake yakiwa Arusha, Tanzania.

TRT Afrika