Bunge la taifa limeidhinisha kutumwa kwa kikosi cha polisi 1000 wa Kenya Haiti / Picha ya Bunge ya Kenya

Bunge la Taifa limeidhinisha kutumwa kwa polisi wa Kenya Haiti. Hatua hii inakuja baada ya mahakama nchini humo kusitisha kwa muda.

Haiti iko katika Bara la Marekani Kaskazini. Katika nchi hiyo, taasisi za serikali zimeacha kufanya kazi kwa ufanisi, na magenge, yanayoungwa mkono na matajiri, yanadhibiti karibu theluthi mbili ya nchi.

Majanga ya asili ya mara kwa mara yanazidisha kuwepo kwa migogoro inayoikabili Haiti.

Kenya imejitolea kuongoza ujumbe wa kimataifa wa usaidizi wa usalama nchini Haiti.

"Wabunge wetu wamekaidi amri ya mahakama," Dkt, Ekuru Auko amesema katika mtandawo wa X.

Aukot ni kiongozi wa chama cha Thirdway Alliance Kenya na ndiye aliwasilisha kesi bungeni akisema uamuzi wa serikali ilikiuka sheria.

Mahakama Kuu ya Kenya ilikuwa imesitisha mipango ya kupelekwa kwa polisi Haiti, huku wakili aliyewasilisha kesi hiyo akidai kuwa hakukuwa na uamuzi wa baraza la mawaziri kuhusu hilo na kwamba bunge lilikuwa likipuuzwa.

" Leo asubuhi tuko mbele ya jaji Mwita katika mahakama ya kwanza kwa ajili ya kusikilizwa kwa ombi hilo. Wakati huo huo, Bunge letu limeuza roho yake kwa Marekani na kwenda kusafisha fujo walizosababisha huko Haiti."

Mwezi Oktoba, Umoja wa Mataifa ulionya kuwa magenge ya kihalifu yanadhibiti maeneo makubwa ya Haiti, na hali ya usalama imeporomoka zaidi, huku idadi ya uhalifu mkubwa ikifikia "rekodi kubwa."

Umoja wa Mataifa unasema kuwa magenge ya kihalifu yameongezeka Haiti / picha AP 

Uamuzi wa serikali kutuma wanajeshi hao umezua utata nchini ikiwa watu wengine wanadai kuwa maafisa wa Kenya wanaweza kuwa hatarini kutokana na kukosekana kwa hali ya usalama nchini Haiti.

"Kwa wale waliofuatilia bunge la taifa leo kwenye mjadala wa Haiti, nina hakika mtakubali kuwa bunge hili letu la 13 ndiyo dhaifu katika muundo wetu wa utawala; Aibu Tu!" mbunge wa Rarieda Otiende Omollo MP ameandika katika akauni yake ya X mara tu baada ya uamuzi huo kupitishwa,

Wananchi wengine wamedai kuwa Haiti ni mbali sana na Kenya na labda ingekuwa bora ikiwa nchi jirani zingetuma vikosi vya usalama badala ya Kenya.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Kithure Kindiki amesema Kenya haitapeleka maafisa hao 1000 wote kwa pamoja, watapelekwa kwa awamu tofauti.

"Bajeti ya kutuma ujumbe Haiti ni dola milioni 600, kwa mwaka mmoja, kama Umoja wa Mataifa utafanya uamuzi," Kithure Kindiki Waziri wa Mambo ya Ndani aliiambia kamati ya bunge wiki iliyopita.

Serikali inasema tayari imetumia dola za Marekani milioni 241 kuandaa baadhi ya maafisa wa polisi waliotengwa kwa ajili ya kutumwa Haiti.

TRT Afrika