Uturuki: Altun anaishutumu Israeli kupotosha umakini wa watu kutoka 'mauaji ya kimbari' Gaza

Uturuki: Altun anaishutumu Israeli kupotosha umakini wa watu kutoka 'mauaji ya kimbari' Gaza

Kuchaguliwa hakumpi mtu yeyote haki ya kutekeleza utakaso wa kikabila, anasema Fahrettin Altun.
Altun alikosoa kampeni ya kijeshi ya Israel huko Gaza, ambayo imedondosha zaidi ya "tani 70,000 za mabomu katika kipindi cha miezi sita, sawa na mabomu kadhaa ya nyuklia." / Picha: AA

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Uturuki ameishutumu serikali ya Israeli kwa kujitahidi kupotosha umakini wa watu kutoka kwa "mauaji ya kimbari" ya Wapalestina.

Kupitia mtandao wa kijamii siku ya Jumatano, Fahrettin Altun alidai kuwa Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu anajaribu kuhalalisha hatua za serikali yake huko Gaza - mauaji ya kiholela, uhalifu wa kivita, na kupuuza waziwazi sheria za kimataifa - kwa kusisitiza kwamba kadhia yake ni ya haki.

"Serikali ya sasa ya Israeli inajaribu sana kupotesha umakini wa watu kutoka kwa mauaji yake ya kimbari dhidi ya Wapalestina.

Waziri Mkuu wa Israeli anathubutu kuhalalisha mauaji ya kiholela ya serikali yake, uhalifu wa kivita na ukiukaji wa sheria za kimataifa kwa kudai sababu za haki. Hakuna mtu, ikiwa ni pamoja na Waisraeli wengi, wanaonunua maneneno haya tena.

Netanyahu amekuwa akitumia shambulio la Oktoba 7 (2023) kama kisingizio cha kuwaua raia wa Palestina na kuwafurusha kutoka katika ardhi zao," alisema.

Alizidi kumkosoa Netanyahu kwa kutoa shutuma zisizo na msingi dhidi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) Karim Khan, kufuatia mikutano ya Khan mjini New York na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan na Rais wa Palestina Mahmoud Abbas, kando ya Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa wiki hii.

"Leo, ana hofu kwamba kesi dhidi yake katika ICC inakwenda kumwandama. Ulinzi wa kidiplomasia wa baadhi ya serikali za Magharibi hautamhakikishia uhuru wa kushtakiwa chini ya sheria za kimataifa. Serikali ya Israeli tayari ina hatia mbele ya macho ya watu wengi, uchunguzi wa ICC utathibitisha tu kile ambacho tayari kinajulikana. Kujaribu kudhoofisha kesi hii kunaweza tu kukubalikai kwa serikali chache za Magharibi ambazo zinashiriki katika mauaji haya ya kimbari," Altun aliongeza.

Kukanusha shutuma za Netanyahu kwamba ICC inawalenga viongozi wa Israeli bila ya haki kama wahalifu wa kivita. Altun alisisitiza kuwa historia tayari imehukumu vitendo hivi, na ni suala la muda tu kabla ya kuwajibishwa.

Alisema kuwa kuchaguliwa hakutoi uhalali wa kutekeleza mauaji ya kikabila, akisisitiza kwamba chini ya uongozi wa Netanyahu, katika mwaka uliopita zaidi ya raia 42,000 wameuawa, mamilioni ya watu kuyakimbia makazi yao, na mamia ya waandishi wa habari kuuawa.

Altun pia alikosoa vita vya Israeli dhidi ya Gaza, ambavyo vilisababisha kurushwa kwa zaidi ya "tani 70,000 za mabomu katika kipindi cha miezi sita, sawa na mabomu kadhaa ya nyuklia."

Alisisitiza dhamira ya Uturuki ya kutafuta haki kwa Wapalestina na kusema kwamba wataendelea kupigania amani na uhuru katika eneo hilo.

TRT World