Katibu Mtendaji wa Baraza la mitihani Tanzania (NECTA) Dr Said Mohamed akitangaza matokeo./Picha: Wengine

Baraza la mitihani Tanzania(NECTA) linasema jumla ya watahiniwa 484,823 ambayo ni sawa na asilimia 87.65 ya waliofanya mtihani wa kidato cha nne wamefaulu.

Kati ya hao, idadi ya wasichana ni 257, 892 wakati wavulana ni 226,931, waliofanya mtihani huo uliofanyika Novemba na Disemba mwaka jana.

Kwa mujibu wa Katibu Mtendaji wa NECTA Dr Said Mohamed, kiwango cha ufaulu kwa mwaka huu kimeongezeka kwa asilimia 1.57 kwa watahaniwa wa shule, ukilinganisha na mwaka 2022.

Wakati huo huo, NECTA imewafutia matokeo watahiniwa 102 kwa sababu za udanganyifu.

Baraza hilo pia limefuta matokeo ya watahiniwa wengine watano baada ya kuandika matusi kwenye karatasi za kujibia mitihani.

Hii si mara ya kwanza kwa baraza hilo kufikia maamuzi kama haya.

Mapema mwaka huu, NECTA iliwafutia matokeo wanafunzi 178 wa darasa la nne na 28 wa kidato cha pili kwa udanganyifu.

Vile vile, baraza hilo limebatilisha matokeo ya wanafunzi watatu wa darasa la nne na 14 wa kidato cha pili, kwa kuandika matusi.

TRT Afrika