Ukiwa na kisukari au diabetes, mwili wako hautengenezi insulini ya kutosha, homoni inayodhibiti sukari ya damu. / Picha: AFP

Huku dunia ikiadhimisha siku ya ugonjwa wa kisukari (diabetes) duniani Shirika la Afya Duniani, WHO, linasisistiza umuhimu wa serikali zote kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu kwa waathiriwa.

Wataalamu wa afya wanasema ukiwa na kisukari au diabetes, mwili wako hautengenezi insulini ya kutosha au hauwezi kuitumia inavyopaswa.

Insulini ni homoni inayodhibiti sukari ya damu.

WHO inasema ni muhimu kuongeza ufahamu wa njia ambazo watu wenye ugonjwa wa kisukari wanaweza kupunguza hatari ya ugonjwa huo.

Shirika la Afya Duniani linasema kuwa ni muhimu watu kujua kuwa kuna aina ya kisukari ambayo haiwezi kuzuiwa.

Aina ya pili ya kisukari mara nyingi huzuilika kupitia lishe bora, mazoezi ya mwili mara kwa mara, kudumisha uzito wa mwili na kuepuka matumizi ya tumbaku.

"Ugonjwa wa kisukari unaweza kuwa tofauti kwa kila mtu, kila uzoefu unaoishi ni muhimu," shirika la WHO limesema,

Shirika la Afya Duniani-WHO linasema kuna zaidi ya watu milioni 24 barani Afrika ambao wanaishi na ugonjwa huu ambao una athari mbalimbali za kiafya kwa mwanadamu.

Zifuatazo ni baadhi ya dalili za Kisukari

-Kuhisi kiu sana

• Kuhitaji kukojoa mara nyingi zaidi kuliko kawaida

• Macho kutoona vizuri

• Kuhisi uchovu

• Kupunguwa uzito ghafla bila kukusudia

Jinsi ya kujikinga na ugonjwa huu

Wataalam pia wanashauri kuwa ni vyema kuamua kujitahidi kufikia uzito unaofaa wa mwili.

• Kufanya mazoezi ya viungo kwa angalau dakika 30 za mazoezi ya wastani kila siku

• Kula chakula cha afya na kuepuka sukari na mafuta mengi.

• Kutovuta sigara.

TRT Afrika