Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) Felix Tshisekedi, amesema kuwa “vitendo vya Rwanda” vinastahili vikwazo vya kimataifa.
"Kinachohitajika kwa sasa ni kumdhibiti mshukiwa mwenyewe wa uhalifu, ambaye ni Rwanda," alisema Rais Tshisekedi siku ya Ijumaa katika Mkutano wa mambo ya usalama mjini Munich nchini Ujerumani.
Kauli ya Tshisekedi inakuja wakati waasi wa M23, wanaoungwa mkono na Rwanda wakizidi kupiga hatua kuelekea jiji la Bukavu.
Mapema Februari 14, waasi hao waliripotiwa kutwaa uwanja wa ndege wa Kavumu, ambao uko kilomita 25 kutoka mji wa Bukavu, makao makuu ya jimbo la Kivu Kusini.
Kufungwa kwa uwanja wa ndege
Kwa sasa, uwanja huo ambao mara nyingi hutumika na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na majeshi, umefungwa kwa muda usiojulikana, huku majeshi ya DRC yakiondoa vifaa vyake kutoka eneo hilo.
Kulingana na msemaji wa taasisi yenye uhusiano wa karibu na M23, waasi hao walikuwa wanaushikilia uwanja huo wa ndege pamoja na maeneo jirani.