Safari za ndege zilicheleweshwa na zingine kughairiwa nchini Kenya mnamo Septemba 11, 2024 baada ya wafanyikazi wa uwanja wa ndege wa JKIA kugoma. / Picha: AFP

Wafanyakazi wa uwanja wa ndege nchini Kenya wamesitisha mgomo wa siku moja uliotatiza safari za ndege kote Afrika Mashariki baada ya kukubali kurejea kazini.

Mgomo huo ulioanza Jumanne usiku wa manane, ulisababisha kusitishwa kwa safari za ndege, zikiwemo zile za RwandAir na mashirika mengine ya ndege ya kanda hiyo, na kuwaacha mamia ya abiria wakiwa wamekwama.

Muungano wa Wafanyakazi wa Usafiri wa Anga nchini (KAWU) ulitangaza kusitisha mgomo huo Jumatano jioni baada ya mazungumzo ya faragha na maafisa wa wizara ya uchukuzi.

Katibu Mkuu wa KAWU, Moss Ndiema aliwaambia waandishi wa habari kuwa wafanyakazi wa uwanja wa ndege "hawaungi mkono mpango wa Adani, kurudi kwao kazini ni kwa masharti, na tumepewa mamlaka ya kupinga makubaliano wakati wowote ikiwa hayaendani na maslahi ya wafanyakazi."

'Pendekezo tu'

Mkataba wa Adani uliokusudiwa na Ndiema ni kuhusu upinzani wa KAWU kwa mpango uliopendekezwa na serikali wa kukodisha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) kwa kampuni ya India, Adani Group.

Msemaji wa serikali Isaac Mwaura alisema Jumatano kwamba "biashara hio ya Adani ya JKIA ni pendekezo tu."

Aliongeza kuwa makubaliano ya kurejea kazini yamefikiwa katika mkutano huo ulioongozwa na Waziri wa Uchukuzi Davis Chirchir.

Uchukuzi uliopangwa, ambao ulilenga kuleta uwekezaji mkubwa kwa ajili ya uboreshaji wa viwanja vya ndege, ulizua shutuma kutoka kwa wafanyakazi wanaohofia kupoteza kazi na mabadiliko ya mazingira ya kazi.

Uwanja wa ndege huhudumia zaidi ya watu milioni 8 kila mwaka

Mgomo huo unakuja baada ya Mahakama Kuu kuamua kusitisha kwa muda mpango uliopendekezwa, ambao ulitaka kukodisha uwanja wa JKIA kwa miaka 30 kwa Adani ili kuwekeza dola bilioni 1.85 ili kuboresha na kupanua uwanja wa ndege.

Licha ya uamuzi wa mahakama, wafanyikazi wa Adani Group wamesalia kwenye uwanja wa ndege, na hivyo kuzidisha mvutano wa wafanyikazi, huku KAWU ikielezea wasiwasi wao.

Uwanja huo wa ndege huhudumia zaidi ya abiria milioni 8.8 kila mwaka lakini umekumbwa na changamoto za miundombinu, ikiwa ni pamoja na kuvuja kwa paa, kukatika kwa umeme mara kwa mara, na vifaa viliyozeeka.

TRT Afrika