Jaji mkuu wa Kenya Martha Koome alifanya maamuzi haya baada ya mkuu wa mashtaka kuomba mawaidha kuhusu kesi ya mwana siasa wa upinzani Martha Karua na wakili Ahmednassir/ Picha: X ya Martha Koome

Mahakama ya juu ya Kenya imesema kuwa maamuzi yake hayawezi 'kupinduliwa' na Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki (EACJ).

" Katiba pia inaipa Mahakama ya Juu mamlaka ya mwisho kuhusiana na tafsiri na matumizi ya masharti yake. Pia, tunasisitiza kuwa maamuzi ya Mahakama ya Juu ya Kenya hayatopitiwa wala kubatilishwa na EACJ," alisema Jaji Koome katika maamuzi yake.

"Hii ina maanisha kuwa Mahakama ya Juu haitoweza kukata rufaa kwenye Mahakama ya EACJ, kwani mamlaka hiyo haina uwezo wa kukagua wala kupitia maamuzi ya Mahakama ya Juu."

EACJ ilianzishwa mwaka 2001 ikiwa na jukumu la kuhakikisha kuwa sheria zote ndani ya nchi wanachama zinatafsiriwa kulingana na mkataba wa kuanzishwa kwa jumuiya hiyo.

Pia hutoa maoni na ushauri wa kisheria, pamoja na kujihusisha kwenye usuluhishi.

Koome alifanya mamuzi haya baada ya mkuu wa mashtaka kuomba mawaidha kuhusu kesi ya mwana siasa wa upinzani Martha Karua na wakili Ahmednassir.

Bi Karua aliwasilisha kesi yake katika mahakama ya kikanda baada ya Mahakama ya Juu kutupilia mbali ombi lake la 2017 la kupinga kuchaguliwa kwa Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru.

Yeye na wakili wa Uganda Male Mabirizi pia waliwasilisha kesi nyingine mbele ya EACJ kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais wa Agosti 9, 2022, mara tu baada ya Mahakama ya Juu kutupilia mbali maombi kadhaa ya kupinga ushindi wa Rais William Ruto katika kura zilizoshindaniwa

Kwa upande wake, Wakili mashuhuri nchini Kenya, Ahmednassir Abdullahi aliwahi kwenda kwenye Mahakama hiyo inayopatikana jijini Arusha, Tanzania, akipeleka shauri la ukiukwaji wa haki mbalimbali ukiwemo ule wa kuipinga Mahakama ya Juu ya Kenya baada ya kumuwekea pingamizi la muda usiojulikana kutokana na mashambulizi yake ya mara kwa mara dhidi ya majaji wa mahakama hiyo ya juu zaidi.

" Kwa hivyo, Mkataba wa EAC ni sehemu ya sheria za Kenya ambazo lazima ziwe chini ya Katiba na ikiwa kuna mgongano wowote kuhusu uongozi wa mahakama za Kenya na mahakama zilizoundwa na Mkataba huo, masharti ya Katiba huchukua nafasi ya kwanza kuliko yale ya Mkataba wa kikanda," Jaji mkuu Koome aliongeza.

Pata habari zaidi kupitia whatsapp channels

TRT Afrika