Utamaduni wa Harambe eumelaumiwa kutekwa na wanasiasa wanaotaka kuficha fedha za wizi au kuzitakasa / Picha : TRT Afrika

Na Dayo Yussuf

Harambee. Ni neno. Sio lazima kusema chochote kabla au baada, inajisimamia yenyewe kama sentensi.

Ni njia ya Wakenya ya kuwaita watu pamoja ili kusaidiana.

Umati wa watu hukusanyika kila baada ya muda fulani katika vijiji, makanisa, viwanja vya jamii au hata majumbani, ili kuchangisha fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo kama vile hospitali, barabara, au hata kutafuta fedha kwa ajili ya bili za hospitali au karo ya shule.

Mila iliyoota mizizi tangu wakati wa uhuru.

Baba mwanzilishi Mzee Jomo Kenyatta anasifiwa kwa kuanzisha utamaduni huo wakati ambapo Kenya ilikuwa ikifanya ujenzi na maendeleo.

‘’Baada ya uhuru, Harambee iliwekwa ili kuhakikisha kuwa jamii inaweza kushiriki katika ujenzi wa taifa pamoja na kila mmoja kwa ajili ya maendeleo,’’ asema Profesa Kennedy Ongaro, mwanasosholojia na mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Daystar jijini Nairobi. ‘’Kiini cha moyo wa Harambee kilikuwa kusaidia Taifa kuwaondoa maadui watatu wa maendeleo: Umaskini, magonjwa na kutojua kusoma na kuandika,’’ Profesa Ongaro anaiambia TRT Afrika.

Kwa miaka mingi, nchi ilifanikiwa chini ya uwajibikaji wa pamoja wa Wakenya. Watu waliisaidia serikali, huku maofisa wa serikali wakijitokeza pia kusaidia watu.

‘’Mimi binafsi nilinufaika na Harambee. Shule yangu ya msingi ilijengwa kupitia ufadhili wa Harambee. Pia nilipelekwa Chuo Kikuu nje ya nchi kwa hali hiyo hiyo,’’ anasema Profesa Ongaro.

Lakini sasa, Harambee inashambuliwa.

Kizazi cha Gen Z walipoingia mitaani nchini Kenya, mojawapo ya madai waliyotoa ni kupigwa marufuku kwa uchangishaji fedha za umma na maafisa na viongozi wa serikali.

Hili walisema limekuwa njia ya kufuja pesa walizopata viongozi wafisadi.

‘’Wanasiasa hawa hawa na watu mashuhuri katika jamii wanatembea na mikoba iliyojaa pesa. Michango ya mamilioni ya pesa katika michango kote nchini. Lakini hawawezi hata kueleza jinsi au wapi walipata pesa hizo,’’ anasema Prof Ongaro.

Serikali ya Kenya imepiga marufuku viongozi wa serikali kutoa michango kanisani / Picha: Reuters 

Lakini msumeno unakata pande mbili linapokuja suala la pesa hizi za Harambee. Watu pia wamelalamika kuhusu wahisani hao kutumia michango yao kwa manufaa ya kibinafsi.

‘’Kenya ndiyo ilipo leo kwa sababu Gen Z wameona kwamba taasisi za kidini zimeoza hadi msingi. Wanaruhusu majukwaa yao kutumiwa na wanasiasa kuficha pesa zao zilizoibwa kwa jina la michango,’’ Prof Ongaro aliambia TRT Afrika.

Siku moja tu baada ya maandamano ambayo yaligeuka kuwa ya vurugu na vijana wa Kenya, rais William Ruto alitangaza kwenye Televisheni ya Taifa ya kupiga marufuku mara moja kuchangisha pesa za Harambee haswa na maafisa wa serikali.

Lakini hii haikuchukua muda mrefu, kwani Bw Ruto huyo alionekana Jumapili iliyofuata, akichangia shilingi nusu milioni kwa kanisa alikohudhuria ibada katika eneo la Kati mwa Kenya.

Wengi wanaojiita mamilionea wanaohudumu katika baraza la mawaziri la Bw Ruto wameonekana katika miezi ya hivi majuzi wakitoa michango ya kejeli makanisani na kuchangisha pesa taslimu. Katika mifuko, mifuko mikubwa maarufu kama Ghana must go.

Tangu wakati huo wote wamefukuzwa kazi.

''Hatuna miundo, hatuna fomula, hatuna sera inayoeleza ni kinyume cha sheria kufanya jambo moja, mbili tatu hivi, kwa hivyo unaweza kufanya chochote na kila kitu nchini Kenya kwa jina la Harambee na hakuna uwajibikaji mwisho wa siku,'' asema Prof Ongaro. ‘’ Na ndiyo maana watu hawafurahishwi na ari hii ya Harambee,’’ anaongeza.

Waumini wanachangisha pesa katika msikiti mjini Omdurman, Sudan / Picha : Kumbukumbu reuters 

Zaidi ya kutumiwa kama kauli mbiu ya kuchangisha pesa, imeongezeka maradufu kama kitia-moyo kwa watu kuvuta kazi pamoja kimwili, labda wakati wa kuinua vitu vizito au kufanya kazi fulani.

Lakini kulingana simulizi za kale Harambee inatoka kwa Wahindi wa kwanza waliokuja kufanya kazi kwenye Reli ya Afrika Mashariki wakati wa utawala wa kikoloni.

Ilikuwa mchanganyiko wa mungu wa Kihindu Hare, na Ambe, mungu wa kike wa nguvu na nishati.

Iwe msukumo wa kibinadamu au nguvu ya kiroho, Wakenya wengi wanategemea sana utamaduni huu wa Harambee. Je, marufuku hii ya maafisa wa serikali kutoa michango kama hii, itasaidia kusafisha sifa ya Harambee kwa mara nyingine tena?

TRT Afrika