Nchini DRC wataalam wanahofia kuwa watoto katika makambi ya wakimbizi wako katika hatari ya kupata Mpox / Picha: Reuters

Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) imezitaka nchi wanachama kutoa elimu kwa wananchi wao jinsi ya kujikinga na kuzuia kuenea kwa ugonjwa wa Mpox (Monkeypox).

Hii ni kufuatia ripoti za Shirika la Afya Duniani (WHO) kuwa Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) zinakabiliwa na mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya Mpox.

Burundi imethibitisha kesi tatu (3) za Mpox huko Bujumbura na Isare, zilizothibitishwa na maabara za kitaifa na WHO.

Wizara ya Afya ya Burundi imewahakikishia wananchi kwamba hatua zipo katika kudhibiti ugonjwa huo, huku wagonjwa kwa sasa wakipata matibabu na kuonesha kuimarika.

Tangu 2022, DRC imeripoti zaidi ya kesi 21,000 na zaidi ya vifo 1,000, kulingana na WHO. Mnamo 2023, kulikuwa na kesi 14,626 na vifo 654, na hadi mwisho wa Mei 2024, kesi 7,851 na vifo 384 viliripotiwa.

Wengi wa walioambukizwa ni watoto chini ya miaka mitano (39%), na karibu theluthi mbili (62%) ya vifo pia ni miongoni mwa watoto.

Wataalamu wa afya wanasema wamegundua aina mpya ya virusi katika sehemu moja ya nchi. Burundi inapakana na DRC, Rwanda na Tanzania huku DRC ikipakana na nchi tano washirika wa EAC: Tanzania, Burundi, Rwanda, Uganda na Sudan Kusini.

TRT Afrika