khamenei / Photo: Reuters

Hezbollah iliitaka Iran katika siku za hivi karibuni kuanzisha mashambulizi dhidi ya Israel huku mapigano kati ya kundi la wanamgambo wa Lebanon na jeshi la Israel yakiongezeka kwa kasi, lakini Iran hadi sasa imejizuia, maafisa wawili wa Israel na mwanadiplomasia mmoja wa nchi za Magharibi waliiambia Axios.

Kulingana na ripoti hio, maafisa wawili wa Israeli walisema maafisa wa Iran waliwaambia wenzao wa Hezbollah kwamba "muda si sahihi" wa kuanzisha mashambulizi dhidi ya Israel kwa sababu rais wa Iran Masoud Pezeshkian kwa sasa yuko New York kwa ajili ya Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa.

Maafisa wawili wa Israeli na mwanadiplomasia mmoja wa nchi za Magharibi waliiambia Axios kwamba ujasusi wa Israeli na Marekani unaonyesha kuwa Hezbollah iliifikia Iran katika siku za hivi karibuni na kuwataka Wairani kusaidia kwa kufanya shambulio la kulipiza kisasi mauaji ya Israeli ya kiongozi wa Hamas Ismail Haniyeh katika mji wa Tehran miezi miwili iliyopita.

Hata hivyo Jeshi la Israeli siku ya Jumatatu 25.9.2024, lilitoa wito kwa wakaazi wa kusini mwa Lebanon kuhama mara moja majumba na majengo mengine ambapo lilidai Hezbollah inahifadhi silaha na kusema ilikuwa ikifanya "mashambulio makubwa" dhidi ya kundi hilo la wanamgambo.

Lilikuwa ni onyo la kwanza la aina yake katika takriban mwaka mmoja wa mzozo unaozidi kuongezeka mara kwa mara na lilikuja baada ya majibizano makali ya moto siku ya Jumapili.

Hezbollah ilirusha takriban roketi 150, makombora na ndege zisizo na rubani kaskazini mwa Israeli kulipiza kisasi kwa mashambulizi yaliyomuua kamanda mkuu na makumi ya wapiganaji.

Hezbollah imeapa kuendeleza mashambulio yake kwa mshikamano na Wapalestina na Hamas.

TRT Afrika na mashirika ya habari