Rais Erdogan atoa rambirambi kwa wana wa Ismail Haniyeh. / Picha: AA

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amewapokea Abdusselam na Hammam Haniyeh, watoto wa mkuu wa ofisi ya kisiasa ya Hamas Ismail Haniyeh, ambaye aliuawa na Israel mwezi uliopita katika mji mkuu wa Iran Tehran.

Wakati wa mkutano wa Jumamosi, Erdogan alitoa rambirambi zake kwa wana wa Haniyeh kutokana na kifo cha baba yao.

Mkuu wa Shirika la Kitaifa la Ujasusi la Uturuki (MIT) Ibrahim Kalin na Mshauri Mkuu wa Rais Sefer Turan pia walikuwepo.

Ismail Haniyeh aliuawa Julai 31, katika mji mkuu wa Iran Tehran.

Mauaji ya Haniyeh

Iran na kundi la wapiganaji wa Palestina Hamas wameilaumu Israel, ambayo haijathibitisha wala kukana kuhusika.

Hata hivyo, kwa mujibu wa ripoti ya vyombo vya habari, Israel iliufahamisha utawala wa Marekani kwamba ndiyo iliyohusika na mauaji ya kiongozi wa chama cha politburo cha Hamas Ismail Haniyeh tarehe 31 Julai katika mji mkuu wa Iran Tehran.

"Wakati Israel imekataa kutoa maoni yake kuhusu mauaji ya Haniyeh, iliwafahamisha maafisa wa Marekani mara baada ya hapo kwamba ilihusika," gazeti la Washington Post liliripoti Jumanne, likiwanukuu watu watatu wanaofahamu mawazo ya Ikulu ya Marekani, lakini bila kutaja majina yao.

"Maafisa wa Ikulu ya Marekani walijibu kwa mshangao na hasira kwa mauaji ya Haniyeh ya Julai 31, ambayo waliona kuwa yanarudisha nyuma azma yao ya miezi kadhaa ya kupata usitishaji vita huko Gaza," gazeti hilo lilisema.

TRT World