Erdogan alisisitiza kwamba kuunga mkono Palestina na Lebanon si tu jukumu la kimaadili kwa Waislamu bali ni msimamo wa ubinadamu, amani na utamaduni wa kuishi pamoja miongoni mwa imani tofauti. /Picha: AA

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amefahamisha kuwa Uturuki imewasilisha tani 30 za misaada ya kibinadamu kwa Lebanon, na mipango ya kuendelea kutoa msaada kadiri hali ya usalama itakavyoruhusu.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari mjini Ankara siku ya Jumatano, Rais Erdogan alisisitiza kujitolea kwa Uturuki kusaidia wale walioathiriwa na migogoro inayoendelea katika eneo hilo.

"Ulimwengu wa Kiislamu lazima uwe na jibu kali zaidi kwa ukandamizaji huko Gaza, Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu na Lebanon. Kama Waislamu, ni jukumu letu kuuongoza ulimwengu katika kukomesha ukatili huu," Erdogan alisema, akizitaka mataifa ya Kiislamu kuungana dhidi ya dhuluma zinazowakabili Wapalestina na Walebanon.

Erdogan alisisitiza kwamba kuunga mkono Palestina na Lebanon si tu jukumu la kimaadili kwa Waislamu bali ni msimamo wa ubinadamu, amani na utamaduni wa kuishi pamoja miongoni mwa imani tofauti.

"Leo hii, kusimama kwa ajili ya Palestina na Lebanon kunamaanisha kusimama kwa ajili ya ubinadamu wote," alisema.

Katika matamshi yake, Erdogan amelaani vitendo vya kile alichokitaja kuwa ni "Wazayuni wachache wenye itikadi kali" ambao chuki na ghasia zao zinavuruga eneo na kutishia amani ya dunia. "Wakiwa wamepofushwa na damu na chuki, wanaichoma moto eneo hilo na dunia nzima. Hatutakubali ukatili na ushenzi huu," alitangaza.

Rais wa Uturuki pia alitoa wito kwa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuchukua hatua za haraka, akirejea azimio la mwaka 1950 la 'Kuungana kwa ajili ya Amani', ambalo liliwezesha matumizi ya nguvu katika maeneo yenye migogoro.

Erdogan alilitaka baraza hilo kupendekeza hatua kama hizo kwa Gaza kusitisha ghasia na kuwalinda raia.

TRT World