Jackline Chepkoech wa Kenya ameshinda mbio za mita 3000 kuruka viunzi kwa kukimbia muda wa dakika 8:57.35 Picha : Twitter  IAAF 

Muethiopia Gudaf Tsegay ameshinda mbio za mita 5000 za wanawake London, katika mzunguko wa mwisho wa ligi ya Wanda Diamond.

Gudaf Tsegay, ambaye pia ni bingwa wa dunia wa1500m, na 3000m, alivunja rekodi ya mzunguko wa mbio hizo kwa kukimbia kwa muda wa dakika 14:12.29.

Mkenya Beatrice Chebet, alimaliza wa pili na kuboresha muda wake binafsi kwa kukimbia muda wa dakika 14:12.92 kwenye kitengo kilichowakutanisha bingwa wa Olimpiki, bingwa wa dunia na gwiji wa Diamond League.

Ingawa alimaliza katika nafasi ya tatu, Bingwa wa Olimpiki, Mholanzi Sifan Hassan alivunja rekodi ya Uropa kwa kuweka rekodi mpya ya muda wa dakika14:13.42.

Jackline Chepkoech wa Kenya ameshinda mbio za mita 3000 kuruka viunzi kwa kukimbia muda wa dakika 8:57.35 ambao ni muda unaongoza zaidi duniani katika kitengo hicho.

Aidha, mkimbiaji chipukizi wa Ethiopia Medina Eisa amevunja rekodi ya dunia kwa wanariadha chipukizi wasiozidi miaka 20, (U20) kwa kukimbia muda wa dakika 14:16.54.

TRT Afrika