Vilabu vya soka barani Afrika viko mbioni hatua ya kufuzu kuwa kati ya vilabu 16 bora vitakavyopangwa hatua ya makundi. Picha: CAF

Michuano ya kufuzu kwa hatua ya pili ya mechi za kutinga kwa makundi ya Kombe la Mabingwa kwa wakilishi wa Tanzania Yanga na KMKM na kombe la shirikisho CAF, Singida Fountain Gate, JKU na Azam FC, inatarajiwa kuamua hatma ya wawakilishi wa Tanzania kwenye mashindano ya CAF msimu huu.

Singida Fountain Gate FC imekaribia raundi ya pili ya hatua ya mchujo kwa kuikung'uta JKU FC 4-0 na iwapo itaruka viunzi, itapiga dhidi ya Future FC ya Misri.

Mabao mawili ya Marouf Tchakei ikiwemo penalti, Morice Chukwu na bao la Mkenya Duke Abuya kwenye kipute cha Uwanja wa Azam Complex yamezidisha nafasi ya Singida Fountain Gate FC kwenye mashindano hayo.

Hata hivyo, KMKM ililazwa 2-1 nyumbani na St. George ya Ethiopia na kuwa na kibarua kuukwea mlima kwenye mechi ya marudio baada ya mabao ya Biniyam Belay na nahodha Natnael Zeleke kuzidisha matumaini ya mabingwa wa Uhabeshi huku wakijiandaa kuilaki KMKM katika uwanja wa Ababa Bikila chini ya majuma mawili.

Wawakilishi wengine wa Tanzania kwenye Ligi ya Mabingwa CAF, Yanga watajitosa uwanjani jumapili dhidi ya ASAS Djibouti Telecom kutoka Djibouti lakini sasa, kinyume na awali, iwapo timu itatemwa hatua ya raundi ya pili ya mchujo, haitopokewa Kombe la Shirikisho na badala yake, itaaga mashindano hayo ya bara.

Azam FC imetua Addis Ababa, Ethiopia, salama na kushiriki mazoezi yake Uwanja wa Abebe Bikila, tayari kutoa burudani dhidi ya Bahir Dar Kenema siku ya Jumapili katika Uwanja huo wa Abebe Bikila.

Maandalizi ya Azam yamepigwa jeki baada ya kisiki Yannick Bangala kurejea kikosini kufuatia jeraha ya misuli ya paja.

Iwapo Yanga itachupa hadi hatua ya pili, itapambana na mshindi wa mechi kati ya Al Merrikh ya Sudan na AS Otoho ya DRC.

Kwa upande wako, wekundu wa Msimbazi, Simba SC, itavaana na bingwa kati ya Power Dynamos ya Zambia na African Stars FC

Kulingana na ratiba ya hatua ya awali ya mechi za mkondo wa pili, ngoma hizo zimepangwa kuanzia Septemba 15-16 huku mechi za marudiano zikichezwa Septemba 29-20.

TRT Afrika