Emmerson Mnangagwa, 80, atahudumu kwa muhula wa pili kama rais wa Zimbabwe baada ya kushinda uchaguzi wa urais wa Agosti 23, 2023. / Picha: Reuters

Rais wa sasa wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa ametangazwa mshindi wa uchaguzi wa urais wa Agosti 23, 2023 uliovutia wagombea 11.

Tume ya Uchaguzi ya Zimbabwe ilitangaza Jumapili kwamba Mnangagwa mwenye umri wa miaka 80 wa chama cha Zimbabwe African National Union - Patriotic Front (ZANU-PF) alipata kura 2,350,711 (52.6%) ili kupata ushindi wa awamu ya kwanza.

Mpinzani wake wa karibu, Nelson Chamisa mwenye umri wa miaka 45 wa chama cha Citizens Coalition for Change (CCC), aliibuka wa pili kwa kupata kura 1,967,343 (44%).

"Mnangagwa Emmerson Dambudzo wa chama cha ZANU-PF anatangazwa kuwa Rais aliyechaguliwa kihalali wa Jamhuri ya Zimbabwe," Jaji Priscilla Chigumba, mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zimbabwe, alisema wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika mji mkuu wa Harare.

'Kufufua uchumi'

Jumla ya wapiga kura 4,468,668 walipiga kura zao kati ya wapiga kura 6,623,511 waliojiandikisha nchini Zimbabwe, na hivyo kumaanisha waliojitokeza kuwa 68.9%, tume ya uchaguzi ilisema.

Wakati wa kampeni, Mnangagwa aliahidi kufufua uchumi wa Zimbabwe huku kukiwa na mfumuko mkubwa wa bei na sarafu dhaifu ya ndani.

Katika uchaguzi wa Agosti 23, upinzani nchini Zimbabwe, ukiongozwa na Chamisa, ulidai kufanywa udanganyifu na kumpendelea Mnangagwa, tuhuma ambazo tume ya uchaguzi na chama cha ZANU-PF zilikanusha.

Promise Mkwananzi, msemaji wa chama cha CCC cha Chamisa, alisema "watakataa matokeo yoyote yaliyokusanywa kwa haraka bila kuthibitishwa ipasavyo."

'Ushindi wa watu'

“Tutawashauri wananchi hatua zinazofuata kadiri hali inavyoendelea. Hatutakubali kupokonywa ushindi wa watu,” alisema kwenye mtandao wa kijamii wa X, ambao zamani ulijulikana kama Twitter.

Mngangagwa alichukua wadhifa wa urais kwa mara ya kwanza Novemba 2017, akimrithi Robert Mugabe wa muda mrefu ambaye alilazimika kuondoka madarakani baada ya miaka 37 madarakani. Wawili hao walikuwa marafiki wakubwa kabla ya kutofautiana baadaye.

Mnangagwa, mwanachama wa chama cha ZANU-PF, aliendelea na kuibuka kama mshindi wa uchaguzi wa rais utakaofanyika Julai 30, 2018.

Alipata kura milioni 2.46 (51.44%) na kujinyakulia ushindi wa raundi ya kwanza dhidi ya Nelson Chamisa, aliyepata kura milioni 2.15 (45.07%) na kuambulia nafasi ya pili.

Katika uchaguzi wa rais wa Zimbabwe, mgombea anahitaji zaidi ya 50% ya kura ili kutangazwa mshindi wa moja kwa moja.

Iwapo hakuna hata mmoja wa washiriki atakayefikia idadi hii , duru ya pili itafanyika kati ya wagombeaji wawili wa juu.

Kwa mujibu wa sheria, matokeo ya uchaguzi wa urais lazima yatangazwe ndani ya siku tano baada ya kupiga kura.

TRT Afrika