Mshambuliaji wa kujitoa mhanga anasemekana kulipua vilipuzi na kuacha maafa na majeruhi. / Picha: AFP

Kundi la wanamgambo la Al Shabaab limetoa taarifa likidai kuwa ndio limevamia Chuo cha Kijeshi cha Jaalle Siyaad kilichoko mji mkuu wa Mogadishu likiwalenga wanajeshi wa Brigedi ya Oktoba 14 waliokuwa wakijiandaa kwa shughuli zao za kila siku.

Aidha, kundi hilo linadai kuwaua makumi ya wanajeshi na kuwajeruhi askari zaidi, pamoja na kusababisha hasara. Vyombo vya habari vya ndani viliweka majeruhi kuwa zaidi ya watu 30.

Mshambuliaji wa kujitoa mhanga inasemekana kajiipua na bomu na kuacha maafa na majeruhi mapema leo huku shambuilizi hilo likishuhudia mlipuko mkubwa uliofuatwa na milio ya risasi iliyosikika katika maeneo mengi ya mji mkuu wa Mogadishu.

Mkuu mmoja wa usalama mjini Mogadishu, aliliambia shirika la habari la Anadolu, kwa sharti la kutotajwa jina kutokana na vikwazo vya kuzungumza na vyombo vya habari, kuwa mlipuaji wa kujitoa mhanga alihusika katika mlipuko kwenye kituo cha mafunzo ya wanajeshi mjini Mogadishu.

"Mshambuliaji wa kujitoa mhanga aliyejihami, alitekeleza uvamizi wakati wa shughuli nyingi siku ya Jumatatu. Mlipuko ukitokea, kulikuwa na foleni kubwa ya wanajeshi wapya katika kambi ya mafunzo ya kijeshi ya Jalle Siyaad."

Mkuu mmoja wa usalama mjini Mogadishu

Jeshi la Somalia linaendeleza operesheni ya kukabiliana na Al Shabaab na kuwakomboa raia wake kutoka kwa kundi hilo. Aidha, jeshi la Somalia, limesema kuwa limefanikiwa kuwauwa mamia ya wanamgambo na kuwaondoa kutoka maeneo mbalimbali nchini humo.

Kufikia sasa serikali ya Somalia haijatoa taarifa rasmi kuhusu kiasi cha uharibifu uliotokea leo ikiwemo idadi rasmi ya vifo na majeruhi. Hata hivyo, afisa huyo aliongeza kuwa makumi ya watu walijeruhiwa katika shambulio hilo, na kukimbizwa hospitalini kwa matibabu.

TRT Afrika na mashirika ya habari