Makao makuu ya Shirika la Afya Duniani (WHO) jijini Geneva nchini Uswisi./Picha: Getty

Shirika la Afya Duniani (WHO) linajiaandaa kupeleka msaada wa madawa nchini Rwanda, kuisaidia nchi hiyo kukabiliana na ugonjwa huo hatari.

Hatua hiyo inakuja kufuatia kuripotiwa kwa vifo sita nchini Rwanda, siku ya Septemba 28, 2024.

Jumla ya maambukizi 26 na vifo sita vimeripotiwa, kwa mujibu wa WHO.

Maambukizi hayo yameripotiwa katika wilaya saba kati ya 30 nchini humo, huku likiongeza kuwa watu 20 wamewekwa sehemu maalumu za uangalizi wakipokea matibabu.

“Tunaendelea kuandaa mikakati ya kuisaidia Rwanda kudhibiti kusambaa zaidi kwa kirusi cha Marburg,” alisema Dkt Matshidiso Moeti ambaye ni Mkurugenzi wa WHO kwa kanda ya Afrika.

Wakati huo huo, WHO imesema kuwa inaendelea kuratibu namna ya kukabiliana na ugonjwa huo, hasa katika maeneo yanayopakana na Rwanda.

Virusi vya Marburg vinatajwa na wataalamu wa afya kuwa sawa na virusi hatari vya Ebola, vikiwa vimegunduliwa kwa mara ya kwanza mwaka 1967 nchini Ujerumani baada ya watu 9 kuambukizwa na saba kufariki dunia.

TRT Afrika