Tetemeko la ardhi lakumba Johannesburg nchini Afrika Kusini

Tetemeko la ardhi lakumba Johannesburg nchini Afrika Kusini

Majengo katika mji huo yalitikisika baada ya tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 5.0
Tetemeko la ardhi lilitokea karibu na Johannesburg/ Picha: Reuters

Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 5.0 lilitokea Jumapili karibu na Johannesburg, likatikisa majengo katika mkoa wenye idadi kubwa zaidi ya watu nchini Afrika Kusini, kulingana na Ripoti ya Kijiolojia ya Marekani.

Harry Lyimo, mkazi wa Sandton jijini Johannesburg, alisema "Ilikuwa ya kutisha".

"Ardhi ilitetemeka chini ya miguu yangu nilihisi kama vile nimesimama kwenye sakafu ya kiwanda na mitambo ikiendelea kufanya kazi." aliongeza Lyimo.

Tetemeko hilo lilitokea saa 8:38 asubuhi (0038 GMT) umbali wa takriban kilomita 10 (maili sita) chini ya uso wa ardhi, kwa mujibu wa USGS.

Majengo yalitikisika katika mkoa wa Gauteng, ambapo Johannesburg, mji mkubwa zaidi na kitovu cha biashara cha nchi hiyo, ulipo.

Wakazi katika mkoa huo walihisi tetemeko hilo na baadhi walisambaza picha kwenye mitandao ya kijamii zikionyesha uharibifu mdogo wa miundo kama kuta. Hakuna taarifa za haraka kuhusu vifo au majeruhi.

Mwezi Agosti 2014, tetemeko lenye ukubwa wa 5.3 lilitokea karibu na mji wa uchimbaji wa dhahabu karibu na Johannesburg.

Tetemeko kubwa la mwisho kutokea nchini Afrika Kusini lilikuwa ni la ukubwa wa 6.3 na lilitokea mkoa wa Western Cape mwaka 1969.

TRT Afrika na mashirika ya habari