Simba wa Kiafrika ni wa aina yake duniani wakiangaliwa kama ishara ya ujasiri na nguvu/ Picha: Reuters

Na Coletta Wanjohi

Istabul, Uturuki

Simba wa Kiafrika ni wa aina yake duniani wakiangaliwa kama ishara ya ujasiri na nguvu. Wanyama hawa wana miili yenye nguvu—katika familia ya paka, na ni wa pili kwa ukubwa baada ya chui mkubwa mwenye milia yaani tiger —na miungurumo yao inaweza kusikika umbali wa maili tano.

Takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa Tanzania ndiyo inayoongoza kwa idadi kubwa ya simba ikiwa na jumla ya simba 17,000, ikifuatiwa na Afrika Kusini yenye simba 3,284, wakati Botswana inashika nafasi ya tatu ikiwa na simba 3,064.

Kenya nayo inakadriwa kuwa na simba zaidi ya 2500. Hii ni idadi kidogo sana ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka 25 iliyopita.

Simba ndio kwa familia ya paka pekee wanaoishi katika vikundi / Picha: Wengine

Muungano wa Kimataifa wa Uhifadhi wa Mazingira (IUCN) unakadiria kuwa takriban simba 25,000 wamesalia barani Afrika, na ndiyo maana Shirika hilo limeonyesha wasiwasi kuwa simba hao wapo hatarini kutoweka.

Simba ndio paka pekee wanaoishi katika vikundi ingawa kuna idadi moja ya simba wanaoishi peke yao. Fahari ni vikundi vya familia ambavyo vinaweza kujumuisha simba kati ya wawili hadi 40—kukiwa na madume watatu au wanne, majike kumi na mbili au zaidi, na makinda yao.

Simba wa kike ndio wawindaji na viongozi wakuu/ picha: Wengine 

Madume hulinda himaya kwa nguvu zote, wakiweka alama katika eneo hilo kwa mkojo, wakinguruma kwa kutisha ili kuwaonya wavamizi, na kuwafukuza wanyama wanaovamia himaya yao.

Simba wa kike ndio wawindaji na viongozi wakuu. Mara nyingi wanafanya kazi pamoja ili kuwinda swala, pundamilia, nyumbu, na wanyama wengine wakubwa wa mbuga zilizo wazi.

Wengi wa wanyama hawa wana kasi zaidi kuliko simba, kwa hivyo, kazi ya pamoja inaleta faida.Simba jike pia huwalea watoto wake kwa pamoja. Simba wa Kiafrika wanakabiliwa na vitisho mbalimbali—vingi vikihusishwa na wanadamu.

Uwindaji usiosimamiwa hapo awali umesababisha simba kutoweka kutoka katika baadhi ya makazi / picha Getty

Kwa kuhofia kwamba simba watawinda mifugo yao, ambayo inaweza kuwa pigo kubwa la kiuchumi, wafugaji wanaweza kuwaua wanyama hao kwa kulipiza kisasi na kama njia ya kuwazuia, wakati mwengine wakitumia sumu za kuulia wadudu.

Wawindaji haramu wanalenga wanyama hao pia, kwani mifupa yao na viungo vyao vyengine ni vya thamani katika biashara haramu ya wanyamapori. Jukumu la uwindaji wa fahari yaani trophy hunting ni tishio.

Uwindaji usiosimamiwa hapo awali umesababisha simba kutoweka kutoka katika baadhi ya makazi, huku wawindaji na wale wanaohusika na sekta hiyo wakisema ada za uwindaji huzalisha pesa kwa uhifadhi wa simba.

Simba wa Kiafrika huwinda wanyama wakubwa wanaokula majani/ Picha :AP

Kinachochochea zaidi mzozo huu kati ya simba na wanadamu ni upotezaji wa mawindo katika safu ya spishi. Simba wa Kiafrika huwinda wanyama wakubwa wanaokula majani, idadi ya watu ambao wanawindwa kwa ajili ya biashara ya nyama ya porini inayozidi kuwa ya kibiashara.

Kwa kuwa na chakula kidogo kinachopatikana porini, simba wanaweza kuwa na uwezekano mkubwa wa kuwinda wanyama wa kufugwa kama mifugo.

Mbali na kuwa kivutio cha utalii simba ni wawindaji wakuu katika mazingira yao, iwe ni nyika, jangwa au pori wazi/ picha : AP 

Wataalam wanasema kuna umuhimu wa kuwalinda simba wa Afrika kwani mbali na kuwa kivutio cha utalii, simba ni wawindaji wakuu katika mazingira yao, iwe ni nyika, jangwa au pori wazi.

Ina maana kuwa, wanachukua jukumu muhimu katika kuweka uwiano mzuri wa idadi kati ya wanyama wengine, hasa wanyama walao majani kama pundamilia na nyumbu - ambao huathiri hali ya nyika na misitu.

TRT Afrika