Naibu Waziri wa Biashara wa Uturuki Ozgur Volkan Agar amesifu uhusiano wa ukaribu na wa undugu kati ya nchi hizo mbili huku akieleza kuwa Uturuki inafurahia sana mabadiliko makubwa yanayoendelea Sudan. /Picha: AA

Mkutano wa kilele wa Biashara kati ya Uturuki-Sudan na Maonesho ya Uwekezaji wa Uchumi yameanza mjini Istanbul, likileta pamoja maafisa rasmi wa nchi hizo mbili na wafanyabiashara.

"Tunalenga kuendeleza uhusiano wa kibiashara na uwekezaji. Tuko hapa kutatua matatizo yaliyopo kati ya Uturuki na Sudan na kuleta suluhu," alisema Ehlam Mahdi Sabeel, waziri wa uwekezaji na ushirikiano wa kimataifa wa Sudan, alipokuwa akihutubia mkutano huo Jumatano.

"Tunakaribisha kila mwekezaji anayetoka Uturuki kuchangia maendeleo ya Sudan, tunajua kwamba makampuni mengi ya Uturuki yanafanya biashara nchini Sudan na tumetayarisha mazingira ya uwekezaji," alibainisha.

Ozgur Volkan Agar, naibu waziri wa biashara wa Uturuki, pia alisema uhusiano kati ya nchi hizo mbili utaboreshwa kutokana na ushirikiano wa kisekta kama sehemu ya tukio hilo.

Alieleza kuwa ushiriki katika maonesho ya kimataifa, kibiashara, mikataba ya nchi mbili na shughuli nyingine za utangazaji ni muhimu katika kuongeza ushirikiano wa kibiashara na kiuchumi.

Biashara ya kimataifa

Akiashiria kwamba Uturuki inaipa umuhimu maalum bara la Afrika, Agar alisema: "Sudan imekuwa moja ya soko linaloendelea Afrika ikiwa pamoja na rasilimali zake tajiri na nafasi yake ya kimkakati na maendeleo makubwa katika nyanja za kijamii, kiuchumi na kisiasa."

Akisifu uhusiano wa karibu na wa kindugu kati ya nchi hizo mbili, aliongeza kuwa Uturuki ina furaha kubwa na mabadiliko makubwa yanayoendelea Sudan.

"Ningependa kusema kwamba kutokana na kuongezeka kwa nafasi ya Sudan katika biashara ya kimataifa, Sudan inakuwa mshirika wa kibiashara wa kuvutia zaidi kwa mauzo ya nje ya nchi yetu kupitia ushirikiano wake wa kikanda na uwezo wa kiuchumi," alisisitiza.

TRT Afrika