Kulingana na rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, Afrika Kusini bado inafikiria kukata uhusiano na Israeli. /Picha : AA

Afrika Kusini bado inafikiria kukata uhusiano wa kidiplomasia na IsraelI, Rais Cyril Ramaphosa alisema.

Ramaphosa, hata hivyo, alisisitiza uungaji mkono wa Afrika Kusini kwa ajili ya Palestina "hauwezi kubatilishwa."

"Suala hili (kukata uhusiano na Israeli) linazingatiwa kwa njia ya kiutendaji na kwa wakati ufaao litaweza kueleza kwa usahihi maelezo ya kiongozi mkuu kwa azimio ambalo lilichukuliwa na Bunge la Kitaifa," Ramaphosa aliwaambia wabunge Alhamisi.

Rais wa Afrika Kusini aliulizwa kuhusu azimio lililopitishwa na bunge Novemba mwaka jana na kuitaka serikali kukata uhusiano na Tel Aviv kutokana na vita vya Israeli dhidi ya eneo la Gaza, Palestina lililozingirwa.

Akijibu swali la kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters Julius Malema ambaye aliitaja Brazil kumrejesha nyumbani balozi wake kutoka Israeli, Ramaphosa alisisitiza kuwa serikali yake haikuwa ya "kusita" wala "kuogopa."

"Suala hili linazingatiwa na tunazingatia masuala mapana zaidi," Ramaphosa alisema kuhusu azimio lililopitishwa na wabunge, kutaka Ubalozi wa Israeli mjini Pretoria ufungwe.

Akimjibu Rais Ramaphosa, Malema alisema Waafrika Kusini "hawawezi kuwa katika eneo moja na wauaji, wabakaji... (ambao) waliwaua wanawake na watoto na wanataka kuliangamiza taifa la Palestina."

Mwezi Machi mwaka jana, bunge la Afrika Kusini pia lilipiga kura ya kuunga mkono hoja ambayo itapunguza ubalozi wake nchini Israeli kuwa ofisi ya mawasiliano, kufuatia dhuluma zisizo na kikomo dhidi ya Wapalestina.

Afrika Kusini ilianzisha uhusiano wa kidiplomasia na Palestina mwaka 1995, mwaka mmoja baada ya kumalizika kwa utawala wa wazungu wachache.

Tangu wakati huo, Pretoria imekuwa ikikosoa vikali hatua ya Israeli ya kuendelea kuwanyanyasa Wapalestina, ikiwa ni pamoja na sera yake ya muda mrefu ya kujenga vitongoji haramu vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi ya Waarabu katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu.

Afrika Kusini iliwasilisha kesi yake katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki yenye makao yake mjini The Hague mwishoni mwa 2023, ikiishutumu Israel, ambayo imeshambulia Gaza tangu Oktoba mwaka jana, kwa kushindwa kutekeleza ahadi zake chini ya Mkataba wa Mauaji ya Kimbari ya 1948.

Nchi kadhaa zikiwemo Uturuki, Nicaragua, Palestina, Uhispania, Mexico, Libya na Colombia, zote zimejiunga na kesi hiyo iliyoanza kusikilizwa kwa umma mwezi Januari.

Mahakama kuu mwezi Mei iliiamuru Israeli kusitisha mashambulizi yake katika mji wa kusini wa Gaza wa Rafah.

Ilikuwa ni mara ya tatu kwa jopo la majaji 15 kutoa maagizo ya awali ya kutaka kudhibiti idadi ya vifo na kupunguza mateso ya kibinadamu katika eneo lililozingirwa, ambapo idadi ya majeruhi imevuka 42,400.

AA