Tangu Jumamosi, Fidan amefanya ziara rasmi Venezuela na Mexico kujadili uhusiano wa nchi mbili hizi pamoja na maendeleo ya kikanda na kimataifa. / Picha: AA

Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Hakan Fidan na mwenzake wa Mexico Alicia Barcena Ibarra walikutana nchini Mexico na kufanya mazungumzo.

Kulingana na vyanzo vya kidiplomasia vya Uturuki, mkutano kati ya mawaziri Fidan na Barcena ulijadili masuala ya kisiasa, kiuchumi, ulinzi na utamaduni pamoja na uhamiaji, biashara ya binadamu na mapambano dhidi ya ugaidi.

Aidha, walitathmini hali ya Gaza, vita vya Ukraine na maendeleo katika Amerika ya kati.

Mawaziri hao vilevile walijadili hatua zinazoweza kuchukuliwa katika nyanja kama vile utamaduni, taaluma na vijana ili kuboresha ushirikiano ndani ya wigo wa MIKTA, umoja wa Mexico, Indonesia, Korea Kusini, Uturuki na Australia, vyanzo vilisema.

Wakati huo huo, maandalizi ya mkutano wa pili wa Tume ya Pamoja ya Uchumi ya Uturuki na Mexico na Kazi ya Shirika la Ushirikiano na Uratibu la Uturuki (TIKA) huko Mexico kuhusu msaada wa kiufundi pia yalijadiliwa.

Mazungumzo ya kidiplomasia

Kwa upande mwengine, Fidan pia alikutana na Marcela Guerra Castillo, spika wa baraza la wawakilishi la Mexico.

Waziri Fidan amefanya ziara rasmi katika nchi za Venezuela na Mexico tangu Jumamosi, na kujadili uhusiano wa nchi mbili pamoja na maendeleo ya kikanda na kimataifa.

Uhusiano wa kidiplomasia kati ya Uturuki na Mexico ulianzishwa mwaka wa 1927. Mexico ikawa mshirika wa pili wa Kimkakati wa Uturuki katika eneo la Amerika ya Kusini na Karibiani mnamo 2013.

TRT World