Uturuki imewakumbuka waathiriwa wa shambulio la chuki dhidi ya Uislamu lililotokea huko Christchurch huko New Zealand mnamo Machi 15, 2019.
"Katika kumbukumbu ya mwaka wa tano wa shambulio baya la kigaidi lililotekelezwa huko Christchurch, New Zealand mnamo Machi 15, 2019, tunakumbuka kwa heshima wahasiriwa 51, akiwemo raia mmoja wa Uturuki, waliopoteza maisha katika shambulio hilo, na tunawatakia rehema za Mwenyezi Mungu," Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ilisema Ijumaa.
Wizara hiyo pia ilitoa wito kwa jumuiya ya kimataifa "kuchukua msimamo wa pamoja dhidi ya mielekeo dhidi ya Uislamu" katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupambana na chuki dhidi ya Uislamu.
“Tumefurahishwa na kupitishwa kwa azimio leo (15 Machi) na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu hatua za kukabiliana na chuki dhidi ya Uislamu, ambalo tuliliwasilisha pamoja na nchi nyingine wanachama wa Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu,” ilimalizia taarifa hiyo.
Adhabu ya kifungo cha maisha
Mnamo Machi 15, 2019, Brenton Tarrant, gaidi wa Australia, aliua watu 51 na kujeruhi wengine 40 katika Msikiti wa Al Noor na Kituo cha Kiislamu cha Linwood katika jiji la Christchurch.
Alihukumiwa kifungo cha maisha jela mwaka 2020 bila uwezekano wa kupewa msamaha, katika uamuzi wa kwanza kama huo kuwahi kutolewa katika nchi hiyo.
Baadaye, serikali iliunda Tume ya Kifalme ya Uchunguzi ili kujua kama kulikuwa na mapungufu yoyote ya mashirika ya serikali katika shambulio la msikiti wa Christchurch.
Ripoti hiyo ya kurasa 792, ambayo ilichukua takriban miezi 18 kutayarishwa, ilibainisha mapungufu katika mfumo wa utoaji leseni za silaha, pamoja na "mkusanyiko usiofaa wa rasilimali" kwa upande wa mashirika ya usalama.
Ilikuwa imetoa orodha ya mapendekezo, ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya jinsi silaha zinavyodhibitiwa, kuanzisha shirika jipya la upelelezi na usalama la taifa, na pendekezo la polisi kutambua vyema na kujibu uhalifu wa chuki.