"Kusimamishwa kwa ufadhili kwa UNRWA, kufuatia madai dhidi ya wafanyakazi wachache wa UNRWA, kutawadhuru watu wa Palestina," taarifa ya wizara ya mambo ya nje ilieleza. /Picha: TRT World

Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki imeibua wasiwasi kuhusu maamuzi ya hivi karibuni ya baadhi ya nchi za kusitisha ufadhili kwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi wa Kipalestina katika Mashariki ya Karibu (UNRWA).

"Ikifanya kazi katika mazingira magumu sana, UNRWA inakidhi mahitaji muhimu ya mamilioni ya wakimbizi wa Kipalestina," taarifa hiyo ilisema Jumapili.

Ikizungumzia mazingira yenye changamoto ambayo UNRWA inafanya kazi, taarifa ya wizara ya mambo ya nje ilibainisha kuwa tangu Oktoba 7, zaidi ya wafanyakazi 150 wa UNRWA wamepoteza maisha huko Gaza, ikisisitiza hatari zinazowakabili wale waliojitolea kuwasaidia wakazi wa Palestina.

Akitoa wito kwa nchi ambazo zimetangaza kusitisha ufadhili huo kufikiria upya maamuzi yao, "Kusitishwa kwa ufadhili kwa UNRWA, kufuatia tuhuma dhidi ya wafanyakazi wachache wa UNRWA, kutawadhuru watu wa Palestina," ilieleza.

Nchi wafadhili zinazositisha ufadhili kwa UNRWA

Uamuzi wa kusitisha ufadhili kwa UNRWA umekuja kufuatia madai ya Israel kuwatuhumu baadhi ya wafanyakazi wa UNRWA kuhusika katika shambulio la Oktoba 7.

Nchi kadhaa wafadhili, zikiwemo Australia, Uingereza, Finland, Ujerumani na Italia siku ya Jumamosi zilifuata uongozi wa Marekani katika kusimamisha ufadhili wa ziada kwa UNRWA.

Francesca Albanese, ripota maalum wa Umoja wa Mataifa kwa maeneo ya Palestina yanayokaliwa kwa mabavu, alionya kwamba uamuzi wa kusitisha ufadhili kwa UNRWA "unapinga waziwazi" amri ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki ya kuruhusu usaidizi madhubuti wa kibinadamu" kufika Gaza.

Mkuu wa shirika kuu la misaada la Umoja wa Mataifa katika eneo lililokumbwa na vita vya Gaza alionya kwamba kazi yake inaporomoka baada ya nchi tisa kuamua kupunguza ufadhili kwa madai kuwa wafanyikazi kadhaa wa wakala walishiriki katika shambulio dhidi ya Israeli miezi minne iliyopita.

Shirika hilo, ambalo lina wafanyakazi 13,000 huko Gaza, wengi wao wakiwa Wapalestina, ndilo shirika kuu linalosaidia wakazi wa Gaza huku kukiwa na janga la kibinadamu.

TRT World