Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan akikaribishwa na mwana wa mfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman kwa sherehe rasmi mjini Jeddah, Saudi Arabia Julai 17, 2023. / Picha: AA 

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amewasili Saudi Arabia ikiwa ni sehemu ya ziara ya siku tatu ya nchi za Ghuba ya kuimarisha uhusiano wa kikanda.

Katika hatua ya kwanza ya safari yake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudia Faisal bin Farhan Al Saud na maafisa wengine walimkaribisha Erdogan siku ya Jumatatu katika uwanja wa ndege katika mji wa bandari wa Jeddah.

Rais ameandamana na wajumbe wake wa baraza la mawaziri na maafisa wengine wa Uturuki.

Mahusiano ya nchi mbili na masuala ya kikanda na kimataifa yatakuwa kwenye ajenda.

Baada ya Saudi Arabia, Erdogan atazuru Qatar na Umoja wa Falme za Kiarabu.

Kukuza mahusiano

Wakati wa ziara yake katika nchi tatu za Ghuba, Erdogan alisema hapo awali kwamba anataka kuimarisha uhusiano nao na kukamilisha mikataba ya uwekezaji.

Akihutubia mkutano wa wanahabari mjini Istanbul kabla ya kuanza ziara yake ya nchi za Ghuba, Erdogan alisema uhusiano wa kidiplomasia na Saudi Arabia ulianzishwa mwaka 1929.

"Tunataka kupanua misingi imara ya mahusiano yetu hadi eneo pana zaidi la ushirikiano," aliongeza.

Ikiwa ni moja ya nchi muhimu zaidi katika kanda, Saudi Arabia ina nafasi maalum katika maeneo kama vile biashara, uwekezaji na huduma za kandarasi, rais wa Uturuki alisema.

"Thamani ya miradi iliyofanywa na wanakandarasi wetu nchini Saudi Arabia katika miaka 20 iliyopita ni takriban dola bilioni 25. Tungependa makampuni ya Uturuki kuchukua nafasi kubwa katika miradi mikubwa ya Saudi Arabia," aliongeza.

TRT World