Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan akizungumza na waandishi wa habari baada ya sala ya Ijumaa mjini Istanbul / Picha: AA

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amesema kuwa hakuna tarehe iliyowekwa ya ziara inayopendekezwa ya rais wa Urusi Vladimir Putin nchini Uturuki lakini anatumai kuwa rais wa Urusi ataweza kufanya safari hiyo mwezi Agosti.

"Tarehe haiko wazi, lakini waziri wa mambo ya nje, mkuu wa shirika la kijasusi, wote wanafanya mazungumzo," Erdogan aliwaambia waandishi wa habari baada ya sala ya Ijumaa mjini Istanbul. "Katika mfumo wa mazungumzo haya, nadhani ziara hii itafanyika kwa matumaini mwezi Agosti."

Matamshi ya Erdogan yalifuatia maongezi yake ya simu, Jumatano na Putin, ambapo walikubaliana Putin atafanya ziara Uturuki katika siku zijazo.

Erdogan pia alimwambia Putin kwamba Uturuki itaendelea na juhudi zake "za kina" na diplomasia kwa ajili ya kurejesha mkataba wa nafaka wa Bahari Nyeusi.

Mnamo Julai 17, Urusi ilisitisha ushiriki wake katika makubaliano hayo, ambayo ilitia saini mnamo Julai 2022 pamoja na Uturuki, UN, na Ukraine kuanza tena usafirishaji wa nafaka kutoka bandari za Bahari Nyeusi za Ukraine ambazo zilisitishwa baada ya vita vya Urusi na Ukraine kuanza mnamo Februari.

Moscow imelalamika kuwa sehemu ya Urusi ya makubaliano hayo haikutekelezwa.

Uturuki inayosifiwa kimataifa kwa juhudi yake ya kipekee kama mpatanishi kati ya Ukraine na Urusi, imetoa wito mara kwa mara kwa Kiev na Moscow kumaliza vita kwa njia ya mazungumzo. Kuhusu suala la hivi majuzi ya Putin kujitolea kupeleka nafaka katika nchi za Afrika bila malipo, Erdogan alisema:

“Tuko sambamba na Urusi katika suala hili, yaani tutageuza nafaka zinazotoka Urusi kupitia ukanda wa Bahari Nyeusi kuwa unga na tutafanya usafirishaji wa (unga) kwa nchi maskini za Afrika na nchi ambazo hazijaendelea.”

Hata sasa, Uturuki itaendelea kuchukua hatua hizi na kutoa msaada wake kwa nchi maskini, alisema.

Alipoulizwa kuhusu Mali, nchi ya Afrika Magharibi ambayo iliishi chini ya utawala wa kikoloni wa Ufaransa, "kufanya maamuzi mapya na kuanza kupinga hilo," Erdogan alisema:

"Hili sio jambo la kwanza Ufaransa kufanya. Kwa maneno mengine, ni ilichofanya huko Algeria zamani, ilichofanya Rwanda,ilichofanya nchini Mali, yote haya sasa yanapatikana katika rekodi zote za kimataifa. Waafrika wanalijua hili vizuri sana."

Makoloni ya zamani, Erdogan alisema, “sasa yamesimamisha kabisa usafirishaji wa dhahabu, pamoja na usafirishaji wa uranium hadi Ufaransa. Ni matokeo ya nchi hizi kuteswa kwa miaka mingi."

Uturuki inafanya kazi kudumisha uhusiano wake mzuri na nchi za Kiafrika, aliongeza.

Uturuki kwa muda mrefu imesisitiza uhusiano wake na nchi za Kiafrika kwa kuzingatia kanuni ya ushirikiano, tofauti na mtazamo wa jadi wa ukoloni wa nchi za Ulaya, ambao viongozi wa Uturuki wamehimiza kuwa nchi za Ulaya zikiri na kuomba msamaha.

TRT Afrika