Vitabu vya Kiswahili TPH Bookshop Dar es Salaam Tanzanaia vinauzwa kwa wingi | Picha: TPH

Na AAA Majid

Ni kawaida kwa wanadamu kutafuta kujua asili au historia yao kwa usahihi. Moja ya sababu zinazochangia ni pamoja na kutaka kujua mambo ya zamani yalivyokuwa, wakitaka kulinganisha na hali ya sasa na kujaribu kutabiri yajayo.

Katika makala haya, nitaangazia na kuchunguza lugha ya Kiswahili na jinsi ilivyokuja kuwa lugha ya mawasiliano barani Afrika.

Katika siku zijazo, Kiswahili kama lugha kinapaswa kuchukua nafasi kubwa na pana zaidi Afrika. Jambo la kushukuru ni kwamba matumizi ya Kiswahili barani Afrika yamepata msukumo mpya baada ya UNESCO kuitambua na kuitangaza tarehe 7 Julai kama Siku ya Lugha ya Kiswahili Duniani.

Ni hatua ya kuvutia kwa Kiswahili, kwani imeweka rekodi mpya na ya kipekee miongoni mwa lugha za Kiafrika katika bara hili.

Lugha imepata umuhimu mkubwa kiasi kwamba hata vyombo vya habari vinavyotambulika duniani kama vile BBC, DW, VoA, redio ya Ufaransa, Japan, China, redio ya Umoja wa Mataifa, TRT, n.k., vina idhaa maalum za Kiswahili.

Kuna mambo mengine pia yanayochangia kwa kiasi kikubwa kukomaa kwa lugha hii. Mashindano ya michezo, mikutano ya kisiasa na shughuli za kiuchumi huchangia pakubwa katika kukuza lugha.

Lugha ya Kiswahili inazidi kupata umaarufu katika nyanja za kitaaluma. Picha: Reuters

Kombe la Dunia la 2022 nchini Qatar na michuano kama hiyo iliyotangulia nchini Afrika Kusini ni mifano mikubwa ya nafasi lugha hio katika kuwaunganisha wazungumzaji. Katika nyanja za kisiasa, bunge la Afrika Mashariki hutumia Kiswahili katika mijadala yake.

Ukuaji wa lugha ya Kiswahili barani Afrika unachangiwa na urahisi wake katika kujifunza. Hii inathibitika katika sarufi, muundo, na sauti zake. Sasa mataifa mengine yanakubali kwamba ni rahisi kujifunza. Kwa hivyo, wageni hujifunza kwa bidii kidogo tu.

Mashirika kadhaa ya kimataifa yametuma watu katika nchi kama Tanzania na Kenya kujifunza lugha hiyo tangu miaka ya 1960.

Kwa hivyo, Kiswahili hakikomei Afrika tu. Inazidi kupata wasemaji zaidi, hata Ulaya na Amerika. Ripoti kadhaa zinaonyesha kuwa wanafunzi wa Marekani na Ulaya huchagua lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya msingi ya Kiafrika katika masomo yao ya chuo kikuu. Vile vile, kuna ripoti kwamba baadhi ya wanajeshi nje ya Afrika wanajifunza na kufundisha Kiswahili kwa sababu za kiusalama.

Kiswahili ni miongoni mwa lugha 10 bora kati ya lugha 6,000 zinazozungumzwa zaidi duniani. Mbali na hayo, ni mojawapo ya lugha rasmi nchini Tanzania, Kenya, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Lugha ya Kiswahili inafundishwa katika vyuo vikuu barani Afrika. Picha: Reuters

Vyuo vikuu mbalimbali vya Afrika kama vile Afrika Kusini, Rwanda, Malawi, Ghana, Zimbabwe, Burundi, Kenya na Uganda vimeweka lugha ya Kiswahili katika silabasi zao. Mipango zaidi inaendelea ili lugha hiyo itumike nchini Namibia na Afrika Kaskazini. Hakuna lugha nyingine yenye asili ya Kiafrika imepata mafanikio ya pekee kama haya.

Zaidi ya hayo, tarehe 9 Desemba 2022, bendera ya lugha ya Kiswahili ilipandishwa kwenye Mlima Kilimanjaro, mlima mrefu kabisa barani Afrika, kama ishara - sauti yake inapaswa kuenea katika bara zima la Afrika. Kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na sekta binafsi, Prof. Aldin Mutembei wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alisimamia utekelezaji wa azimio hilo.

Bila shaka, kwa kuzingatia hali halisi inayoendelea, juhudi zinafanywa na viongozi wa kisiasa nchini Tanzania, watu wa nje kama vile kiongozi wa upinzani wa Afrika Kusini, Julius Malema na wadau wengine, ili kukifanya Kiswahili kuwa lugha kuu ya mawasiliano barani Afrika.

Lugha ya Kiswahili inafundishwa katika vyuo vikuu barani Afrika. Picha: Reuters

Pamoja na matumaini yaliyoonyeshwa hapa, changamoto za kimsingi bado zinazuia lugha ya Kiswahili kufika maeneo mapana zaidi barani Afrika. Changamoto hizi ni pamoja na fikra potofu zinazoshikiliwa na wasomi, wanasiasa na viongozi barani Afrika. Fikra potofu zenye madhara ni zao la mapungufu ya kifikra na kisaikolojia yanayotokana na athari za ukoloni mamboleo.

Sababu nyingine ni hofu ya kuachwa nyuma na teknolojia mpya, kukosekana kwa uzalendo kwa Waafrika, woga usio na maana au hofu ya kitu chochote kipya au kisichojulikana, umaskini, na mengineyo. Hata hivyo, kuna dalili nyingi kwamba lugha inayozungumziwa leo ni bora kuliko ilivyokuwa zamani kutokana na maendeleo ya sasa ya kiuchumi, kisiasa, na kijamii barani Afrika.

Iwapo hatua madhubuti itachukuliwa leo, Kiswahili kama lugha kinaweza kuwakilisha sauti ya bara la Afrika. Hii ndiyo lugha pekee yenye asili ya Kiafrika yenye uwezo huo.

AAA Majid ni Mhadhiri Msaidizi wa Lugha na Fasihi ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Waislamu Morogoro Tanzania

TRT Afrika