Maziko ya pamoja ya waathirika wa mlipuko wa lori la mafuta uliotokea kwenye jimbo la Jigawa./Picha: Reuters  

Maziko ya pamoja ya waathirika wa tukio la kulipuka kwa lori la mafuta yamefanyika kwenye jimbo la Jigawa nchini Nigeria.

Idadi ya vifo vilivyotokana na mlipuko huo, kwa sasa imeongezeka na kufikia 147, wengi wa waathirika wakiwa ni watoto, idara ya huduma za dharura ilisema siku ya Jumatano.

Tukio hilo lilitokea usiku kaskazini mwa jimbo la Jigawa kwenye mji wa Majiya baada ta dereva wa lori hilo kupoteza mwelekeo na kupinduka, msemaji wa Jeshi la Polisi Lawan Adam alisema. Mamia ya watu walikimbilia eneo la tukio kwa lengo la kuchota mafuta kabla ya "mlipuko mkubwa kutokea.”

Milli mingi ilishindwa kutambulika, kwa mujibu wa idara za uokoaji.

"Watu takribani 140 walizikwa kwenye kaburi moja," mkuu wa Idara ya Taifa katika eneo hilo, Nura Abdullahi, aliliambia Shirika la Habari la Associated Press.

'Wabakia majivu'

Wahanga wengi wa tukio hilo walibakia kuwa majivu, kulingana na Haruna Mairiga, mkuu wa idara ya uokoaji huko Jigawa.

“Laiti kama wangejua hatari iliyokuwa inawasubiri, wasingeenda kuchota mafuta," alisema Mairiga.

Hata hivyo, mkazi mmoja wa eneo hilo aliwaambia waandishi wa habari kuwa moto huo ulisambaa kwa kasi na hivyo kuwawia vigumu kujiokoa. "Watu walikuwa wanakimbia hovyo hovyo, huku wakiomba msaada," alisema Sani Umar.

TRT Afrika