Wizara ya kilimo ya Rwanda inasema kuwa uzalishaji wa chakula kati ya Septemba 2023 hadi Februari 2024 ilikuwa chini ikilinganishwa na msimu huo mwaka uliopita. / Picha: AFP

Serikali ya Rwanda imeanzisha mpango wa kulima kikamilifu ardhi yote kati ya Februari na Juni mwaka huu.

Wizara ya Kilimo nchini Rwanda inasema jitihada hizo zinalenga kuhakikisha uzalishaji wa kutosha wa mazao muhimu nchini, kama vile mahindi, maharage, soya, viazi na ndizi.

Wizara hiyo inasema kuwa uzalishaji kati ya Septemba 2023 hadi Februari 2024 ulikuwa chini ikilinganishwa na msimu huo mwaka uliopita. Inasema majanga yanayohusiana na mabadiliko ya tabia nchi kama vile mafuriko na ukame yaliathiri uzalishaji.

Kwa mfano, kiasi cha uzalishaji wa mahindi kinakadiriwa kuwa tani 446,460, ikilinganishwa na tani 390,879 zilizokadiriwa katika msimu huo wa 2023, kulingana na MINAGRI.

"Kama isingekuwa mvua iliyosababisha uharibifu wa mazao yetu, tungeweza kukabiliana na uhaba wa uzalishaji wa mahindi na kuanza kusafirisha hata kwa mataifa mengine," Ildephonse Musafiri, Waziri wa Kilimo na Ufugaji alisema katika taarifa yake ya kila mwaka.

TRT Afrika