Rwanda inasema kutopeleka kesi zote mahakamani na kutumia mbinu mbadala kumesaidia kuokoa pesa nyingi/ Picha: AP

Rwanda imesifia uamuzi wake wa kutumia mbinu tofauti ya kutatua migogoro mbali na mahakama.

Ripoti ya serikali inaonyesha hii imeifanya serikali kutotumia fedha ambazo zingetumika mahakamani.

Katika muda wa mwaka 2023/2024, zaidi ya kesi 12,000 zilipatiwa ufumbuzi kupitia mbinu za upatanishi na makubaliano na hapo kufanya serikali kuokoa $5,636,551 kutoka kwa mapatanisho 38.

Katika mwaka uliopita 2022/2023 nchi hiyo iliokoa $7,179,091 ( Rwf 9,558,832,028 ) kupitia mbinu mbadala ya kutatua migogoro, huku mwaka uliopita nchi iliokoa $8,261,469 ambayo ni zaidi ya Rwf bilioni 11.

Harrison Mutabazi, msemaji wa mahakama, anasema kuwa katika kipindi cha miaka saba iliyopita, kesi 6,848 zilitatuliwa kwa njia ya upatanishi.

Tangu mwaka wa 2005, zaidi ya mahakama 12,000 za jamii za Gacaca zilijaribu kutatua takriban kesi milioni 1.2/ Picha: Reuters 

Mwaka 2023/2024 pekee ulishuhudia kesi 2,199 zikisuluhishwa kwa njia ya upatanishi na kesi 10,785 kwa njia ya mashauriano, ikionyesha mabadiliko ya kitamaduni kuelekea kusuluhisha mizozo bila taratibu za muda mrefu za mahakama.

"Upatanishi unapunguza muda unaotumika mahakamani, kwani kuna rufaa chache na mchakato wa utekelezaji ni wa haraka," Mutabazi alisema.

Mbinu tofauti za sheria

Mnamo Juni 2012, mahakama za jamii zilizoitwa Gacaca za Rwanda zilifungwa baada ya kushughulikia takriban kesi milioni mbili za uhalifu wa mauaji ya kimbari.

Mahakama hiyo ndio kiini cha juhudi za serikali kufikia umoja wa kitaifa na maridhiano kufuatia ghasia za mauaji ya kimbari ya 1994.

Rwanda ilichagua haki ya ndani, ya kijamii badala ya njia nyengine za upatanishi baada ya migogoro kama vile msamaha au tume za ukweli.

Kwa kushauriana na wafadhili wake wa kigeni, serikali ilizifanya mahakama za Gacaca kuwa utaratibu wake wa kimsingi wa kisheria wa kutoa rekodi ya kweli ya nani alifanya nini kwa nani wakati wa mauaji ya kimbari ya 1994.

Rais wa Rwanda Paul Kagame alielezea mpango huo kama “suluhisho la Kiafrika kwa matatizo ya Kiafrika.”

Tangu mwaka wa 2005, zaidi ya mahakama 12,000 za jamii za Gacaca zilijaribu kutatua takriban kesi milioni 1.2.

TRT Afrika