Mazao yatakayolimwa kati ya Septemba hadi Februari, 2025 ni pamoja na mahindi, maharagwe na soya, / Picha: Reuters

Pato la kilimo nchini Rwanda linatarajiwa kupanda kwa asilimia 10 katika msimu wa kati ya Septemba hadi Februari, 2025. Hii ni kulingana na Bodi ya Maendeleo ya Kilimo na Rasilimali ya Wanyama ya Rwanda (RAB).

“Uzalishaji wa kilimo unaweza kuongezeka kwa asilimia 10 ikilinganishwa na msimu huo wa 2024, lakini hii itategemea pia mwelekeo wa hali ya hewa,” Telesphore Ndabamenye, Mkurugenzi Mkuu wa RAB alibainisha kwa vyombo vya habari.

Mwaka 2023, Rwanda ilirekodi tani 4,063,804 za mazao ya kilimo katika msimu huo, ambayo iliongezeka hadi tani 4,379,725 mwaka 2024.

Kwa kawaida msimu huo huchangia asilimia 70 ya jumla ya mazao ya kilimo ambayo hulisha nchi.

RAB imetangaza kuwa hekta za ardhi zinazotolewa kwa kilimo cha mazao pia zitaongezeka kwa asilimia 10, kama sehemu ya mikakati mipana ya kuongeza uzalishaji wa kilimo.

Mazao mbalimbali yatapandwa kwenye zaidi ya hekta 800,000 katika msimu ujao.

Wastani wa tani 47,000 za mbolea ya madini yenye ruzuku zinapangwa kupewa wakulima pamoja na tani 4,200 za mbegu bora za mahindi, ngano na soya zitasambazwa katika msimu huo.

Mazao yatakayolimwa ni pamoja na mahindi, maharagwe na soya, chini ya mpango wa mzunguko wa mazao. Malisho ya ziada ya ng'ombe pia yatapandwa kwenye ardhi hiyo hiyo.

TRT Afrika