Kipindi cha Ramadhan ndio mwezi mtukufu katika imani ya Kiislam.  Picha: AFP  

Na Firmain Eric Mbadinga

Magatte Ndiaye huanza siku yake na "Ndeki", au kifungua kinywa katika lugha ya Kiwolof nchini Senegal.

Ni utaratibu wake wa kila siku, kama dereva wa watu mashuhuru katika mji mkuu wa nchi hiyo Dakar, bila hata kupata mlo wa mchana.

Kama ilivyo kwa mabilioni ya waislamu wote duniani, Magatte ameanza mfungo wake toka Machi 11, ikiashiria kuanza kwa mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Kama vile mtu yeyote anayefahamu mila za Ramadhan, kijana huyo anafahamu kwamba kula kabla ya jua kuchomoza na baada ya kuzama , katika kipindi hiki kunaleta faida nyingi za kiafya.

Mabadiliko ya kimwili

Katika siku ya kwanza, mtu yeyote anayefunga kama Magatte, nidhamu yake ya lishe inabadilika. Udhibiti wa kimetaboliki ni chanzo cha mabadiliko haya, ambayo hutoa faida zingine nyingi.

"Kufunga wakati wa Ramadhani hudhibiti sukari ya damu na homoni, hukusanya mafuta, na kutakasa mwili. Hukuza ufahamu wa lishe bora na ulaji wa afya kwa muda," mtaalamu wa lishe wa Senegal Jasmina Fall Ndour aliambia TRT Afrika.

"Vijana huendana na mabadiliko kwa haraka sana, na miili yao hufanya kazi kwa ufanisi zaidi huku ikitumia nishati, ambayo inasababisha faida za muda mrefu."

Kwa baadhi ya watu, changamoto huwa ni ya kisaikolojia na udhabiti wa mabadiliko ya lishe.

Tende ndio bidhaa maarufu wakati wa kufuturu katika mwezi mtukufu wa Ramadhan.Picha: AP

"Kitu cha msingi cha kufanya ni kula vizuri kadiri muda unavyoruhusu na kuacha vitu vyenye sukari sukari na mafuta. Pia ni vyema kuwa na virutubisho kwenye milo," Jasmina anashauri.

Kama moja ya nguzo tano za Uislamu, kufunga wakati wa Ramadhan si kujizuia na kula chakula kwa muda maalum. Bali ni ishara ya imani na utii kila Muislamu lazima atekeleze kwa uwajibikaji, ila kwa walioruhusiwa kutofunga.

Kujenga mwili

Jambo la kushangaza zaidi ni namna ya taratibu za kufunga Ramadhani zinavyolingana na mapendekezo ya madaktari.

"Katika suala la iwapo kila mtu anaweza kufunga mwezi wa Ramadhan, ifahamike kuwa madhara ya kufunga yanaweza kutofautiana kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine, kutegemeana na umri na afya kwa ujumla," mtaalamu wa lishe Jasmina anaiambia TRT Afrika.

Kwahiyo, kama hakuna sababu yoyote ya kitabibu kumshauri mtu aache kula kutoka asubuhi mpaka jua linapozama, mwezi wa Ramadhan ni muhimu sana kwa afya ya mtu.

Kwa watu wanaoweza kufunga, wanashauriwa kuudhibiti miili yao, haswa wakati wa siku za mwanzo za mfungo. Shughuli za michezo ambazo zinahitaji nishati nyingi mwilini, hazipendekezwi kipindi cha mwezi mtukufu.

Magatte, ambaye hupenda kucheza soka kama kujifurahisha, ameacha kufanya hovyo katika kipindi hiki.

"Ni muhimu pia kuhakikisha kuwa unakunywa maji ya kutosha katika nyakati zinazoruhusiwa. Vile vile, inashauriwa kuacha michezo yenye kutumia nguvu na yenye kuchosha," anasema Jasmina.

Athari za kula kupita kiasi

Wataalamu wa lishe wanashauri kuweka nidhamu ya kula na kunywa, kila mara mtu anapohisi njaa.

Waislamu wanashauriwa kusoma zaidi Quran wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhan. Picha : AP

"Ni kawaida kuona watu wanakula kupita kiasi na kwa haraka haraka. Hapa Senegal, hilo linaonekana kuwa tatizo," anasema Jasmina.

"Wakati wa kufugua swaumu, ni muhimu kuchagua vyakula vinavyorejesha nishati, kurejesha maji mwilini na kutupatia virutubishi. Ni vyema kuanza taratibu na tende, maji kidogo au chai ya mitishamba na supu nyepesi. Ni bora kuipa kipaumbele matunda badala ya chakula kingi."

Muhimu ni kuchukua muda wa kutafuna chakula badala ya kumeza chakula. "Kwa nini usitumie nyakati za maombi kama mapumziko?" anapendekeza mtaalamu huyo wa lishe.

Kulingana na mtaalamu huyo wa lishe, msisitizo usiwe kwenye idadi ya chakula au kiasi chake, lakini ubora wa chakula.

"Kitu cha muhimu zaidi ni kuacha kula chakula kwa wingi. Hicho ndio kitu cha muhimu. Unatakiwa kuweka kipaumbele vyakula kidogo na vilivyo bora," anasema.

Kufunga swaumu katika Uislamu sio tu kujizuia kula na kunywa, pia kunahusisha kutojamiiana wakati unafunga.

Waislamu pia wanatakiwa kujitolea muda zaidi kusoma Quran na kuswali swala za usiku.

TRT Afrika