Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak anakabiliwa na changamoto kwa mipango yake ya kuwahamisha baadhi ya wanao omba hifadhi nchini Rwanda/ Picha: Wengine

Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak alikabiliwa na changamoto ya mipango yake ya kuwahamisha baadhi ya waomba hifadhi nchini Rwanda baada ya Bunge la Juu la Uingereza kuunga mkono kuwa utekelezaji wa sheria ya kuidhinishwa kwa mkataba huu ucheleweshwe.

Chini ya mpango wa Rwanda, ambao bado haujatekelezwa, waomba hifadhi wanaofika katika pwani ya kusini mwa Uingereza kwa boti ndogo watapelekwa Rwanda.

Katika jitihada za kuepukana na upinzani wa mahakama ambayo imesema mpango huo ni kinyume cha sheria, Uingereza ilitia saini mkataba na Rwanda mwaka jana, ambapo ilikubali kushughulikia masuala ya usalama, na serikali inajaribu kupitisha sheria kupitia bunge.

Ingawa mawaziri wanaweza kuchukua hatua za kupuuza hoja hiyo, wabunge katika Bunge la Juu waliunga mkono kura ya kupinga mswada huo kwa kura 214 dhidi ya 171.

Sunak amesema anataka safari za kwanza za ndege zianze kuondoka miezi michache ijayo - kabla ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa katika nusu ya pili ya mwaka huu - ili aweze kutimiza moja ya ahadi zake tano za "kusimamisha boti."

Serikali ilipitisha sheria ya Rwanda katika Bunge la Chini wiki iliyopita baada ya siku kadhaa za mjadala ulioonyesha mgawanyiko mkubwa katika chama tawala cha Conservative.

Bunge la Juu la Uingereza linatarajiwa kujadili mswada huo kwa mara ya kwanza mwishoni mwa Januari huku kura nyingi zikitarajiwa kutokea mwezi Machi.

Wabunge hawa wanaweza kuongeza marekebisho kwenye sheria na wanaweza kuchelewesha mswada huo kwa mwaka mmoja, na hii itamaanisha kuwa hauwezi kupitishwa hadi baada ya uchaguzi ujao.

TRT Afrika