Zaidi ya Wapalestina 13,300 wameuawa na mashambulizi ya anga ya Israel huko Gaza. / Picha: AA

Afrika Kusini itaandaa Jumanne mkutano wa kilele wa kundi la mataifa ya BRICS, akiwemo Rais wa Urusi Vladimir Putin, kujadili vita vya Israel-Hamas, Pretoria na Moscow zilisema Jumatatu.

BRICS - Brazil, Russia, India, China na Afrika Kusini - ni kundi la mataifa makubwa yanayoinukia kiuchumi yanayotaka kuunda upya utaratibu wa kimataifa usiotegemea Marekani na Magharibi.

Siku ya Jumanne "Mkutano wa kipekee wa Pamoja kuhusu Hali ya Mashariki ya Kati huko Gaza" utaandaliwa na Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa kwa matumaini ya kuandaa jibu la pamoja kwa mzozo huo uliodumu kwa zaidi ya wiki sita.

Viongozi kutoka Saudi Arabia, Argentina, Misri, Ethiopia, Iran na Umoja wa Falme za Kiarabu - ambao wote wanastahili kujiunga na kundi la BRICS Januari 2024 - watahudhuria mkutano huo.

Mkuu wa Umoja wa Mataifa kushiriki

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres pia atashiriki, ofisi ya rais wa Afrika Kusini ilisema katika taarifa yake.

Iliongeza kuwa wakuu wote watano wa nchi za BRICS watajiunga na mkutano huo wa kilele, ambapo baada ya hapo taarifa ya pamoja yenye marejeleo maalum ya Gaza inatarajiwa.

Mapigano yanaendelea huko Gaza baada ya Hamas kufanya mashambulizi dhidi ya Israel mnamo Oktoba 7. Takriban watu 1,200 walikufa, kulingana na rekodi za serikali ya Israeli.

Huko Gaza, karibu watu 13,300, zaidi ya 5,500 kati yao wakiwa watoto, wameuawa katika mashambulizi ya kulipiza kisasi angani na ardhini, maafisa katika eneo linaloongozwa na Hamas wamesema.

Kuunga mkono Palestina

Afrika Kusini kwa muda mrefu imekuwa ikiunga mkono hoja ya Palestina, huku chama tawala cha African National Congress (ANC) mara nyingi kikihusisha na mapambano yake dhidi ya ubaguzi wa rangi.

Alhamisi iliyopita, ANC ilisema kwamba itaunga mkono hoja ya bunge ya kusitisha uhusiano wa kidiplomasia na Israel hadi ikubali kusitishwa kwa mapigano huko Gaza, ikilaani "vitendo vya mauaji ya halaiki ya utawala wa Israel."

Siku ya Ijumaa, Afrika Kusini iliungana na mataifa mengine manne katika kuitaka uchunguzi wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu kuhusu mzozo wa Israel na Hamas.

China kihistoria imekuwa ikiwahurumia Wapalestina na kuunga mkono suluhu la mataifa mawili katika mzozo wa Israel na Palestina.

TRT Afrika