Takriban waandishi wa habari 38 wameuawa na mashambulio ya bomu ya Israel walipokuwa wakiripoti ukatili wa Tel Aviv kutoka Gaza ya Palestina tangu Oktoba 7/ Picha: AFP

Mpiga picha wa TRT Hamzeh Naaji amekamatwa na polisi wa Israel, bila maelezo yoyote, wakati wa matangazo ya moja kwa moja kwa TRT Arabi, huko Jerusalem Mashariki inayokaliwa kwa mabavu na Israel.

"Juhudi zetu zinaendelea kuhakikisha mwenzetu ameachiliwa," Mkurugenzi Mkuu wa TRT Zahid Sobaci alisema kwenye X kufuatia kukamatwa kwa Naaji siku ya Ijumaa.

"Licha ya ghasia za Israel dhidi ya waandishi wa habari, sauti ya Palestina haitanyamazishwa," Sobaci aliongeza.

Mashtaka dhidi ya Naaji, ambaye ana kadi ya GPO iliyotolewa na Israel, hayajafichuliwa na maafisa, na mwanahabari huyo anatarajiwa kufikishwa mahakamani tarehe 4 Novemba.

Naibu Mkurugenzi Mkuu Omer Faruk Tanriverdi pia alilaani mashambulizi ya Israel dhidi ya waandishi wa habari, akisema kukamatwa huko ni "mbinu ya wazi ya vitisho dhidi ya waandishi wa habari wanaofanya kazi katika eneo hilo."

Akidai kuachiliwa kwa Naaji mara moja, Tanriverdi alisema Shirika la Utangazaji la Uturuki lilikuwa linafuatilia kwa karibu hali hiyo kwa uratibu na mamlaka rasmi zinazohusika.

Kwenye akaunti rasmi ya X ya Shirika hilo, TRT ilisema "Kukamatwa huko ni onyo kwa waandishi wa habari wanaofanya kazi katika eneo hilo."

Takriban waandishi wa habari 38 wameuawa kutokana na mashambulizi ya mabomu ya Israel walipokuwa wakiripoti ukatili wa Tel Aviv kutoka Gaza ya Palestina tangu Oktoba 7.

TRT Afrika