Rais wa zamani wa Malawi, Peter Mutharika / Picha: AFP

Chama Kikuu cha upinzani nchini Malawi, siku ya Jumapili kimemuidhinisha kiongozi wa zamani wa nchi hiyo Peter Mutharika kama mgombea wake katika uchaguzi wa Rais utakaofanyika mwakani.

Mutharika, mwenye umri wa miaka 84, ambaye alipata kuhudumu kama Rais kuanzia 2014 hadi 2020, alisema katika hotuba yake ya kukubali nafasi hiyo kuwa, yeye na chama chake watarekebisha uchumi ambao ukuaji wake umekuwa wa upungufu wa fedha na kukabiliwa na uhaba wa fedha za kigeni uliosababisha ukosefu wa mafuta na dawa.

Mutharika atakabiliana na Rais aliye madarakani Lazarus Chakwera kutoka chama cha Malawi Congress Party, ambaye naye atakuwa anawania kuongoza kwa muhula wa pili katika uchaguzi utakaofanyika Septemba 16, 2025.

"Tumezoea kushinda dhidi ya upinzani. Tutafanya vivyo hivyo mwaka ujao. Tunakuja kurekebisha uchumi," Mutharika aliuambia mkutano mkuu wa chama chake mjini Blantyre.

Chama cha Chilima

Mutharika, profesa wa zamani wa sheria, alisimamia uboreshaji wa miundombinu na kupungua kwa mfumuko wa bei wakati wa uongozi wake, lakini wakosoaji walimshutumu kwa rushwa na urafiki, madai ambayo ameyakanusha .

Chakwera, mwenye umri wa miaka 69, aliingia madarakani akiahidi kukabiliana na ufisadi na kuharakisha ukuaji wa uchumi, lakini wapinzani wake wanasema hajafanikiwa kwani uchumi wa taifa hilo la kusini mwa Afrika bado ni tete.

Chama cha UTP kilimsaidia Chakwera kumshinda Mutharika kwenye uchaguzi wa mwaka 2020 , lakini kilitangaza kujiondoa katika muungano huo baada ya kifo cha Makamu wa Rais.

UTM bado haijathibitisha muungano na chama cha Mutharika, ambacho kingeipa kinyang'anyiro hicho taswira tofauti.

TRT Afrika