ECOWAS ilikuwa imetishia kutumia nguvu dhidi ya viongozi wa mapinduzi/ Picha : Others 

Na Ishaq Khalid

Masharti ya wiki moja yaliyotolewa kwa viongozi wa mapinduzi ya Niger na Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS, kurejesha utulivu wa kikatiba yamemalizika huku mawingu mazito ya mapinduzi hayo yakiendelea kutanda Niger.

ECOWAS ilikuwa imetishia kutumia nguvu dhidi ya viongozi wa mapinduzi na kumrejesha madarakani rais aliyeondolewa madarakani Mohamed Bazoum iwapo serikali ya kijeshi itashindwa kuachia madaraka ifikapo mwisho wa uamuzi huo Jumapili Agosti 6.

Muda umepita, viongozi wa mapinduzi wnaonekana kutoyumba na ECOWAS inaonekana kuwa katika hali ya kutatanisha kuhusu wazo la kutumia nguvu za kijeshi.

‘’Kuna haja ya kutumia hekima kwa sababu rais aliyeondolewa madarakani na baadhi ya viongozi bado wanashikiliwa na jeshi la serikali,’’ Abdullahi Yalwa, mchambuzi wa masuala ya usalama katika nchi jirani ya Nigeria aliiambia TRT Afrika.

Yalwa anaamini kuwa watawala wa kijeshi wanaweza kumtumia rais aliyezuiliwa kama chanzo cha kutishia kupewa mahitaji yao.

’’ ECOWAS ina nia ya kurejesha utaratibu wa kikatiba lakini jinsi itakavyotekeleza lengo hili bado ni gumu. Moja ya kanuni zake muhimu ni kushikilia demokrasia katika Afrika Magharibi na kukabiliana na mapinduzi ya kijeshi.

Kiongozi wa mapinduzi alikuwa mkuu wa walinzi wa rais nchini Niger Abdourahmane Tchiani  Picha: Others 

Kabla ya mapinduzi ya Niger, Mali, Burkina Faso na Guinea zilikuwa zimeangukia kwa watawala wa kijeshi.

Kutuma majeshi

Hali hiyo ilitokea zaidi ya wiki mbili tu baada ya mwenyekiti mpya wa ECOWAS na rais wa Nigeria Bola Tinubu kuonya kwamba chombo hicho cha kikanda ‘’haitaruhusu mapinduzi baada ya mapinduzi Afrika Magharibi.’’

Majibu yake kwa mapinduzi ya Niger ni tofauti ikilinganishwa na mapinduzi ya awali katika eneo hilo hasa kuhusu tishio la kuingilia kijeshi.

Mara ya mwisho ECOWAS ilitumia uingiliaji kati wa kijeshi kutekeleza demokrasia ilikuwa 2017.

Hapo ndipo ilipotuma wanajeshi nchini Gambia na kumlazimisha rais wa wakati huo Yahya Jammeh kutoroka baada ya awali kupendekeza kuwa hataachia madaraka licha ya kushindwa katika uchaguzi na mgombea wa upinzani Adama Barrow.

Bazoum alichaguliwa mwaka 2021 na kuashiria mabadiliko ya kwanza ya kidemokrasia nchini Niger / Picha:Others 

Hakukuwa na mapambano ya kijeshi katika kesi hiyo.

Linapokuja kwa suala la mapinduzi kwa kawaida chombo hicho huweka vikwazo kama njia ya kulazimisha kurejea kwa demokrasia kama inavyoonekana Mali, Burkina Faso na Guinea.

Rais aliyeng'olewa madarakani Mohamed Bazoum alichaguliwa mwaka wa 2021 na kuashiria mabadiliko ya kwanza kabisa ya nchi hiyo kutoka serikali moja iliyochaguliwa kidemokrasia hadi nyingine tangu uhuru wake kutoka kwa Ufaransa mwaka 1960.

Mapinduzi hayo yanaonekana kuwa kikwazo katika hatua hiyo muhimu.

Maoni ya raia

Ingawa uongozi wa ECOWAS ungetaka uingiliaji wa kijeshi nchini Niger, nchi wanachama zimegawanyika waziwazi kuhusu suala hilo.

Hii ni changamoto kubwa, kulingana na Yalwa.

‘’Hata familia ya ECOWAS imegawanyika. Hii ina maana hakutakuwa na nguvu ya kutisha,’’ mtaalamu huyo wa masuala ya usalama anasema.

Majirani watatu wa Niger, Mali, Burkina Faso na Chad tayari wameweka wazi kuwa hawataunga mkono uingiliaji wowote wa kijeshi.

Chad si mwanachama wa ECOWAS lakini ina uhusiano mzuri na jumuiya hiyo kwa miaka mingi.

Maelfu ya watu walijitokeza barabarani kueleza hisia zao dhidi ya Wafaransa baada ya mapinduzi hayo/ Picha: Reuters

Mali na Burkina Faso, ambazo ni wanachama wa jumuiya ya kikanda na pia chini ya utawala wa kijeshi kufuatia mapinduzi, zimeenda mbali zaidi na kuonya kwamba kikosi chochote cha kijeshi dhidi ya Niger kitachukuliwa kuwa ''tangazo la vita'' dhidi yao pia.

Hii ni ishara ya wazi zaidi ya mgawanyiko.

Nchi hizo mbili zilituma wajumbe ‘’kuonyesha umoja’’ na serikali ya Niger siku moja baada ya tishio ya ECOWAS kwa serikali kuu kukamilika.

Viongozi wa kupindua serikali Niger walitangaza kufungwa kwa anga kwa sababu ya ‘’tishio la kuingilia kijeshi.’’

Pia wamehamasisha watu wengi kuingia mitaani.

Kama inavyoonekana katika mapinduzi ya awali katika eneo hilo, hali ya Niger inaweza kuchukua miezi kadhaa au zaidi kutatuliwa lakini mazungumzo hayo hatimaye yatakuwa njia ya kutoka, Abdullahi Yalwa anaamini.

Uingiliaji kati wa kijeshi hautatoa matokeo yanayotarajiwa.

"Hata ikiwa nguvu itatumika, mazungumzo yatakuwa mwisho,’’ Yalwa adokeza. Mchambuzi huyo wa masuala ya usalama anaamini kuwa ECOWAS inaweza kubadili mapinduzi ya Niger kwa ‘’mtazamo unaojumuisha wote,’’

Rais wa Nigeria Bola Tinubu kama mwenyekiti wa ECOWAS aliapa kutumia nguvu dhidi ya serikali ya Niger/ Picha: Others

Akipendekeza kwamba wadau wote wanapaswa kuweka maslahi ya Niger moyoni. Hata hivyo, kushinda imani ya junta baada ya tishio dhidi yake ni kazi kubwa.

‘’Kubadili mapinduzi ni jambo gumu sana lakini pia linawezekana,’’ anasema.

Huku hali ikiwa bado si shwari, macho yote yanaelekezwa kwa ECOWAS kuona ni jinsi gani itaendelea na mipango yake ya kurejesha demokrasia nchini Niger na iwapo katika muda mrefu inaweza kuepusha hali kama hiyo katika mataifa mengine.

Wataalamu wanaonya kwamba wakati ECOWAS na washikadau ndani ya Niger wakijaribu kutafuta suluhu, kuendelea kujihusisha kwa mataifa yenye nguvu duniani kwa maslahi ya kiuchumi na kijeshi katika Sahel kunaweza kuzidisha hali kuwa ngumu zaidi.

TRT Afrika