Uamuzi wa ICJ unaangazia  upanuzi wa makazi ya Israeli na unyonyaji wa rasilimali katika maeneo ya Palestina. / Picha: AFP

Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) siku ya Ijumaa iliamua kwamba maeneo ya Palestina yanayokaliwa kwa mabavu ni "eneo moja," ambao yatalindwa na kuheshimiwa.

Ikisisitiza kwamba kanuni za "The Hague" zimekuwa sehemu ya sheria za kimila za kimataifa, na hivyo zinawawajibisha Israeli, mahakama ilisema, "Ulinzi unaotolewa na Mkataba wa Haki za Kibinadamu hausitishwi katika wakati wa vita au uvamizi."

Ikizungumzia uvamizi wa Israeli katika maeneo ya Wapalestina, mahakama hiyo ilibainisha kuwa "unyonyaji wa maliasili" wa Israel katika ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu "hauendani na wajibu wake" wa kuheshimu haki ya kujitawala ya Wapalestina.

Hasa zaidi kuhusu kufurushwa kwa nguvu huko Mashariki mwa Jerusalem na Ukingo wa Magharibi, mahakama ilisisitiza kuwa sera na mazoea ya Israeli yanakiuka marufuku ya Mkataba wa 4 wa Geneva juu ya kuhamisha kwa nguvu watu wanaolindwa.

"Sera ya ukaliaji wa mabavu ya Israeli inakiuka Mkataba wa 4 wa Geneva," mahakama ilisema.

Mahakama hiyo ilisema sera na matendo ya Israel ni sawa na kunyakua maeneo makubwa ya ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu, na kwamba "haijashawishika" kwamba kujipanua kwa Israel hadi Ukingo wa Magharibi na Jerusalem Mashariki ni jambo la haki.

ICJ pia ilisisitiza kuwa Israeli imeweza kutumia mamlaka kuu juu ya Gaza licha ya kujiondoa kijeshi mwaka 2005.

'Israel lazima ikomeshe ukaliaji wa mabavu'

Ukaaji wa Israel kwa miongo kadhaa katika maeneo ya Palestina ni kinyume cha sheria na unahitaji kukomeshwa "haraka iwezekanavyo", mahakama kuu ya Umoja wa Mataifa ilisema Ijumaa.

"Mahakama imegundua kwamba kuendelea kuwepo kwa Israeli katika Maeneo ya Palestina ni kinyume cha sheria," jaji mkuu wa ICJ Nawaf Salam alisema Ijumaa, na kuongeza: "Israel lazima ikomeshe uvamizi huo haraka iwezekanavyo."

"Mahakama imegundua kuwa Israeli... kuendelea kuwepo katika eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu ni kinyume cha sheria," Salam alisema.

ICJ iliiamuru Israel kulipa "fidia kamili", marejesho na fidia kwa Wapalestina wote kwa "vitendo viovu" chini ya uvamizi huo tangu 1967.

Palestina yapongeza uamuzi wa ICJ

Waziri maalum wa Mambo ya Nje wa Palestina Varsen Aghabekian Shahin, alipongeza "siku kuu kwa Palestina" baada ya mahakama ya juu ya Umoja wa Mataifa kutoa uamuzi kuwa uvamizi wa Israeli uliodumu kwa miongo kadhaa ni kinyume cha sheria.

"Hii ni siku nzuri kwa Palestina, kihistoria na kisheria," aliiambia AFP, akizungumza kwa niaba ya wizara ya mambo ya nje ya Palestina. "Hiki ndicho chombo cha juu zaidi cha mahakama duniani na kimewasilisha uchambuzi wa kina wa kile kinachoendelea kufuatia ukaliaji wa Israeli wa muda mrefu eneo la Palestina na kukiuka sheria za kimataifa."

TRT World