Timu ya Morocco U23. Picha / Morocco FA

Wenyeji Morocco, ambao wemekuwa katika fomu ya kustajaabisha, tangu mwanzo wa ngarambe hizi, wametua fainali bila kufungwa na kujiandikishia ushindi wa mechi zake ikiwemo kuifunga Mali 4-3 kupitia kwenye nusu fainali, kufuatia sare ya 2-2.

"Hakuna kitakachokabidhiwa kwetu kwa urahisi. Wamisri bado hawajafungwa hata bao moja katika michuano hii. Hata hivyo, tulikabiliana nao Novemba mwaka jana na tukajipa matokeo chanya, na ninatumai tunaweza kuiga mafanikio hayo katika fainali," alisema kocha Issame Charai wa Morocco.

Wachezaji wa Misir U23. Picha | CAF

Shangwe inazidi kuongezeka huku mahasimu hao wakitarajiwa kuonyesha ubabe wao dhidi ya Mafarao wa Misri, ambao tayari wamefuzu kwa Michezo ya Olimpiki ya 2024 huko Paris, ikiwa ni mara yao ya 13 kushiriki mashindano hayo.

Safari ya Misri hadi fainali ya leo ilianza baada ya kujihakikishia uongozi wa kundi B, kupitia ushindi wake dhidi ya Mali na Gabon, na kutoka sare na Niger na mwishowe kuilaza Guinea 1-0 kupitia goli la Mohamed Shehata.

Makocha wa pande hizo, Issame Charai wa Morocco na Rogério Micale wa Misri wataongoza timu hizo kwenye fainali itakayoandaliwa katika uwanja wa Prince Moulay Abdullah.

Aidha, timu hizo mbili zitajiunga na Mali, kuiwakilisha Afrika kwenye Michezo ya Olimpiki mjini Paris mwaka ujao.

Hii ni baada ya Mali, chini ya Badara Alou Diallo, kuweka historia kwa kufuzu kwa mara ya kwanza baada ya kusubiri kwa miaka 20, ilipoishinda Guinea 4-3 kupitia mikwaju ya penalti baada ya sare tasa katika Uwanja wa Ibn Batouta

TRT Afrika