Rais wa Urusi Vladimir Putin na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi wakitembea wakati wa mkutano wao katika makazi ya jimbo la Novo-Ogaryovo karibu na Moscow, Urusi Julai 8, 2024. /Picha: Reuters

Na

Hannan Hussein

Tangu vita vya Urusi na Ukraine vilipoanza, India imejaribu kusawazisha uhusiano wake wa kiuchumi na kijeshi na Moscow bila kuhatarisha upinzani mkubwa kutoka kwa Kiev na waungaji mkono wake wa Magharibi.

Juali iliyopita Waziri Mkuu wa India Narendra Modi alifanya safari yake ya kwanza nchini Urusi tangu kuanza kwa vita, wiki hii anazuru Ukraine - safari ya kwanza kama hiyo kufanywa na waziri mkuu wa India katika miongo kadhaa.

Lakini je, India inaweza kutekeleza kitendo chake cha kusawazisha? Na inakumbana na vikwazo gani?

Je huu ni muda muafaka wa ziara ya Modi Ukraine, huku kukiwa na hofu ya kuongezeka kwa msuguano na nchi za Magharibi?

Kuridhisha pande zote mbilli

Wakati India inapozidisha ushirikiano wake wa nishati na kiuchumi na Moscow, ni wazi kwamba ukosoaji kutoka Ukraine na Magharibi utaendelea kuzidi.

Baada ya yote, ziara ya Modi nchini Ukraine ni jaribio la kuridhisha pande zote mbili baada ya ziara yake ya siku mbili huko Moscow mnamo Julai, ambayo Rais Volodymyr Zelenskyy aliikosoa ziara hio na kuitaja kama "kuvunjwa kwa moyo na pigo kubwa kwa juhudi za amani."

Ukraine haiko peke yake katika kushinikiza India. Washington pia inataka New Delhi kuongeza uhusiano wake na Urusi kusaidia kumaliza vita.

Hii itakuwa ni mtihani mkubwa kwa India, ambayo haijashutumu vita vya Urusi nchini Ukraine. Ikiwa itajiweka kwenye mchakato wa amani, ni lazima kumshawishi Rais wa Urusi Vladimir Putin kuzungumza na Zelensky licha ya kuongezeka kwa uvamizi wa Ukraine katika eneo la Kursk la Urusi.

India hadi sasa imekataa kukaribia mistari nyekundu ya Urusi na ile ambayo Ukraine, na Magharibi, zinazingatia kama msingi wao wa makubaliano yoyote ya kudumu ya kumaliza vita.

Angalia Mkutano wa Kilele wa Ukraine mnamo Juni. India ilikataa kuidhinisha matakwa ya nchi za Magharibi kwa ajili ya "uadilifu wa eneo" la Ukraine katika usuluhishi wowote wa amani ili kumaliza vita.

Na bado, Modi anajiandaa kuonyesha kutoegemea upande wowote kwa India huko Kiev, kitendo ambacho kitahitaji zaidi ya maneno ya amani na diplomasia ili kuziridhisha nchi Magharibi. New Delhi haijafanya siri ya kukataa kuchukua nafasi ya mpatanishi wakati wa safari hio, na hivyo kukosa njia mbadala za kupendelea Ukraine.

Chaguo lingine

Zingatia maslahi ya nchi mbili. India inaweza kuendeleza ushirikiano wa sekta mbalimbali na Ukraine katika kilimo, miundombinu, afya, elimu, ulinzi na uchumi, lakini mchango wake katika suluhu iliyojadiliwa bado unaweza kubaki kutokuwa na uhakika.

Hili ni muhimu kwa sababu Modi anaahidi uungaji mkono wowote kwa amani huko Kiev, na anatazamiwa kufanya majadiliano ya kina kuhusu vita nchini Ukraine. Lakini ni ukweli kwamba maslahi ya sasa ya usalama ya Ukraine yanapungua katika ajenda ya India, na haiwezi kumudu kupoteza nia njema ya mshirika wake wa kimkakati aliyejaribiwa kwa muda, Urusi.

Rais wa Marekani Joe Biden na maafisa wengine wanashiriki katika mkutano wa kupitia njia ya mtandao na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi kwenye jengo karibu na Ikulu ya White House huko Washington DC mnamo Aprili 11, 2022. /Picha: (MANDEL NGAN / AFP).

Mienendo ya sasa ya vita inaweka India kwenye hali ngumu. Kuna shaka kubwa huko Moscow kwamba ujasusi wa Magharibi uliwezesha uvamizi wa hivi karibuni wa Ukraine huko Kursk, na kusababisha vitisho vya "vita vya dunia" ikiwa uungaji mkono wa Marekani kwa mashambulio ya Ukraine utaendelea.

Kadiri ya upungufu wa uaminifu kati ya Washington na Moscow unavyoongezeka, India inakabiliwa na kazi ngumu ya kutembea juu ya kamba nyembaba kati ya washirika wake wawili muhimu wa kimkakati.

Lakustaajabisha, ni kuwa masilahi ya kiuchumi na kijeshi yanapendekeza kwmaba India imefanya chaguo lake. Ushirikiano wa sekta nyingi kati ya Urusi na India umeongezeka sana tangu mapema 2022. Leo, Urusi inachangia zaidi ya asilimia 40 ya ununuzi wa mafuta ya India na asilimia 60 ya silaha zake.

Sehemu ya mafanikio ya kiuchumi ya India yamechochewa na matembezi yake ya kidiplomasia: ilihakikisha haichukui hatua ambazo ziliipinga Urusi, huku ikitoa ishara kwa nchi za Magharibi kwamba mafuta na silaha za Urusi ni hitaji la kimkakati kwa New Delhi.

Njia hiyo inaweza kufikia mipaka mpya huko Kiev kwa sababu uvumilivu umepungua ndani ya utawala wa Biden. Tayari imeionya India kutochukulia urafiki wa Marekani "kwa urahisi."

Haiwezi kujitnganisha na Magharibi

India ina sababu nzuri za kuishawishi Washington kwamba ina nia ya dhati ya kusawazisha uhusiano wa Ukraine na Urusi.

Kwanza, ni lazima ionyeshe msimamo mkali zaidi dhidi ya matokeo ya kibinadamu ya vita. Ukimya wa India juu ya kuongezeka kwa idadi ya vifo nchini Ukraine Julai iliyopita uliibua wasiwasi ndani ya utawala wa Biden kwamba mshirika wake mkuu wa kimkakati alikuwa akidhoofisha uungaji mkono wa Magharibi kwa Kiev.

Modi lazima aondoe hisia hiyo kupitia ziara yake wiki hii, na ahadi yake ya "kushiriki mitazamo kuhusu utatuzi wa amani wa mzozo unaoendelea wa Ukraine" inaweza kuwa hatua katika mwelekeo huo.

India pia inategemea uungwaji mkono na ushirikiano wa Magharibi kama vile katika Mazungumzo ya Usalama ya Nchi Nne (QUAD) na Mkakati wa Indo-Pacific unaoungwa mkono na Marekani.

Ushirikiano huu ni muhimu kwa ufuatiliaji wa India wa usalama wa nishati na vyanzo vya kiuchumi katika Asia-Pacific, na New Delhi inapenda kujiweka kama mdhamini wa usalama wa kutegemewa kwa washirika wa Magharibi katika Indo-Pacific.

Lakini matamanio hayo yanaweka mkazo zaidi katika hatua ya India ya kusawazisha. Urusi imeonyesha usumbufu wake kuelekea ushirikiano wa 'QUAD; hapo awali, ikidai kuwa Marekani na washirika wake walikuwa wakivuta nchi zaidi upande wao kwa kuzingatia "kanuni za kupinga Urusi au Uchina."

Hii inawasilisha hali ngumu kwa India, ambayo inafuata sera ya kigeni inayokataa kuonekana inaunga mkono kambi yoyote inayopinga Magharibi au Urusi.

Kwa hivyo, lengo kuu la Modi katika ziara ya wiki hii litakuwa ni kujizuia kuchagua kati ya Ukraine na Urusi huku akitarajia upendeleo wa Magharibi. Hata hivyo, kuongezeka kwa mvutano kati ya Urusi na Magharibi kunatatiza hatua ya India ya kusawazisha, na kuifanya kuwa ngumu kurudhisha pande zote mbili haswa pande ya Ukraine.

Mwandishi, Hannan Hussain ni mtaalamu na mwandishi wa masuala ya kimataifa. Alikuwa Msomi wa Fulbright wa usalama wa kimataifa katika Chuo Kikuu cha Maryland, na alikuwa mshaauti wa Taasisi New Lines Institute for Strategy and Policy ya New Lines huko Washington. Kazi ya Hussain imechapishwa na Carnegie Endowment for International Peace, Georgetown Journal of International Affairs, na Express Tribune (mshirika wa International New York Times).

Kanusho: Maoni yaliyotolewa na mwandishi hayawakilishi lazima maoni, mitazamo na sera za uhariri za TRT Afrika.

TRT Afrika