Waandamanaji hao wanamtaka Waziri Mkuu wa Bangladesh Sheikh Hasina ajiuzulu. / Picha: AFP

Takriban watu 91, wakiwemo maafisa 14 wa polisi, waliuawa na mamia zaidi kujeruhiwa kwa risasi kote Bangladesh siku ya Jumapili wakati wanachama wa chama tawala na polisi wakipambana na waandamanaji wanaomtaka Waziri Mkuu Sheikh Hasina ajiuzulu.

Hali ilipozidi kuwa mbaya, serikali iliongeza muda wa kutotoka nje kwa muda usiojulikana.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Makao Makuu ya Polisi ya Bangladesh huko Dhaka, maafisa 13 wa polisi waliuawa katika mashambulizi ya "kigaidi" katika kituo cha polisi kaskazini magharibi mwa mji wa Sirajganj na mmoja mashariki mwa mji wa Comilla.

Zaidi ya polisi 300 pia wamejeruhiwa katika mashambulizi ya waandamanaji katika vituo mbalimbali vya polisi kote nchini, taarifa hiyo iliongeza.

Mtandao umezimwa

Katika hali hii inayojitokeza, serikali iliamuru kuzimwa kwa mtandao wa simu, huku Facebook na WhatsApp zikiwa zimezuiwa tena, gazeti hilo pia lilisema.

Mapema siku ya Jumamosi, watu wawili, mmoja katika Chattogram na mwingine katika wilaya ya kati ya Gazipur, waliuawa katika mapigano na polisi na wafuasi wa chama tawala cha Awami League.

Mratibu mkuu Nahid Islam siku ya Jumamosi katika mkutano mkubwa katika mji mkuu Dhaka alitangaza vuguvugu lisilo la ushirikiano. Alimtaka Hasina kujiuzulu na kuwajibikia vifo wakati wa maandamano ya wanafunzi.

Vuguvugu hilo la kutoshirikiana limetoa wito kwa wananchi kujiepusha na shughuli zote za kawaida za serikali ikiwemo kulipa ushuru na bili za matumizi, kufunga viwanda na ofisi zote na kuzima usafiri hadi pale serikali ya Hasina itakapojiuzulu.

Mazungumzo

Siku ya Jumamosi, Hasina alisema haki itatendeka kwa wale waliouawa wakati wa maandamano ya wanafunzi na pia akatoa wito wa mazungumzo kumaliza maandamano hayo.

Waandamanaji, hata hivyo, walikataa wito wa mazungumzo.

Jumapili kumekuwa na hali ya wasiwasi kote nchini, huku chama tawala cha Awami League kikihamasisha wafuasi wake kujibu waandamanaji.

Katibu Mkuu wa Upinzani wa BNP Mirza Fakhrul Islam Alamgir Jumapili pia alitoa wito kwa wafuasi kusaidia wanafunzi mitaani.

Katika muda wa wiki tatu zilizopita, taifa la Asia Kusini lenye watu milioni 170 limekumbwa na msukosuko kutokana na maandamano yaliyoongozwa na wanafunzi wakitaka kufanyiwa marekebisho kwa mgawo wa nafasi za kazi serikalini.

Takriban watu 150 waliuawa katika maandamano ya hivi majuzi

Serikali ilisema takriban watu 150 waliuawa katika ghasia za hivi majuzi wakati wa maandamano ya wanafunzi mnamo Julai.

Vyombo vya habari vya ndani, hata hivyo, vilisema zaidi ya watu 266, wengi wao wakiwa wanafunzi, waliuawa na majeraha ya risasi katika mapigano na polisi na wanachama wa chama tawala.

TRT Afrika