Waandamanaji wenye hasira walivamia na kuchoma mahema katika kituo cha matibabu ya Ebola kilichopo mashariki mwa mkoa wa Ituri katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo siku ya Alhamisi, wakijaribu kuchukua miili ya ndugu zao waliofariki dunia kutokana na ugonjwa huo, kwa mujibu wa afisa wa eneo hilo.
Ghasia hizo zilizuka katika Hospitali ya Rwampara, iliyopo pembezoni mwa mji mkuu wa mkowa wa Ituri, Bunia, baada ya familia za waathiriwa wa Ebola kudai miili ya ndugu zao kwa ajili ya kuwazika, wakipinga taarifa kwamba walifariki kutokana na Ebola, kulingana na Luc Malembe, afisa wa eneo hilo.
“Makundi ya watu yalijikusanya nje ya hospitali, na waliponyimwa miili ya ndugu zao, walichoma moto mahema kadhaa yaliyokuwa yakihifadhi wagonjwa wa Ebola, jambo lililosababisha polisi kutumia mabomu ya machozi na kufyatua risasi za onyo,” afisa huyo aliwaambia waandishi wa habari mjini Rwampara.
Malembe alitoa wito wa kuongeza uhamasishaji kwa jamii ili kuielimisha kuhusu ugonjwa huo katika eneo ambalo tayari linakabiliwa na changamoto kubwa za kiusalama.
Ghasia hizo zinafanana na matukio ya mwaka 2020 ambapo vituo kadhaa vya afya vilishambuliwa na makundi yenye silaha pamoja na raia wenye hasira wakati wa mlipuko wa Ebola wa mwaka 2018 mashariki mwa Congo kutokana na kutokuamini wafanyakazi wa afya.
Mlipuko huo wa ugonjwa ulitangazwa rasmi tarehe 15 Mei katika mkoa wa Ituri mashariki mwa Congo.
Tangu wakati huo, mamlaka za afya za Congo pamoja na Shirika la Afya Duniani (WHO) zimeripoti takriban maambukizi 600 na vifo 139 vinavyodhaniwa kusababishwa na ugonjwa huo.
Kuenea kwa Ebola
Mlipuko huo sasa umeenea hadi Kivu Kaskazini na kwa sasa umefika Kivu Kusini. Raia wawili kutoka DRC walioambukizwa na ugonjwa huo wameripotiwa kuwa nchini Uganda.
Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC), Jean Kaseya, aliwataka watu siku ya Alhamisi kufuata kwa makini hatua za kujikinga.
Akizungumza mjini Bunia, alithibitisha tena dhamira ya washirika wa Afrika katika juhudi za kukabiliana na Ebola.
“Tuna timu zenye ari kubwa tayari kazini, zenye utaalamu, na tutaziimarisha ili kudhibiti janga hili,” alisema.
Jumapili iliyopita, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilitangaza mlipuko wa Ebola unaosababishwa na aina ya Bundibugyo kuwa dharura ya afya duniani kufuatia kuongezeka kwa idadi ya maambukizi na vifo mashariki mwa Congo.















