Rais Ruto alisema hazina ya Kitaifa inapanga upya bajeti hiyo ili kuafiki ukweli mpya/ Picha Ikulu Kenya 

Baraza la Mawaziri nchini Kenya lilikutana leo na kuarifiwa kuhusu hali ya usalama nchini kufuatia ghasia za siku kadhaa.

Mkutano huo katika Ikulu ya Nairobi, ambao uliongozwa na Rais William Ruto, uliarifiwa kuwa ingawa ghasia hizo zilianza kama maandamano ya kupinga hatua za ushuru zilizopendekezwa katika Mswada wa Sheria ya Fedha wa 2024, zilitekwa nyara na kuchukuliwa na nguvu za uhalifu.

"Rais alisema serikali lazima sasa ijikite katika kupanga mustakabali mpya wa nchi, akidokeza kwamba lazima mabadiliko makubwa yafanywe ili kuendana na mustakabali huo mpya," taarifa ya Ikulu imesema baada ya mkutano huo.

Baraza la Mawaziri pia liliarifiwa kwamba vyombo vya usalama vimetuliza hali na vinaendelea kufuatilia maendeleo. Wanachama hao waliwapongeza maafisa wa usalama, wakisema kwamba kwa ujumla walifanya kazi kwa uweledi katika mazingira magumu sana.

"Kwa maofisa wowote ambao wanafanya kazi nje ya mipaka ya sheria, Baraza la Mawaziri lilisema watachukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu za kisheria na taasisi zilizopewa mamlaka ya kufanya hivyo," taarifa ya Ikulu imesema.

Baraza la Mawaziri pia limetaka hatua zichukuliwe dhidi ya wale waliofanya uhalifu wa kutisha wa kuchoma moto, uporaji na wizi, miongoni mwa mambo mengine, likisema ukatili kama huo unapaswa kuadhibiwa.

Kuhusu Mswada wa Fedha ulioondolewa, Rais Ruto alisema Hazina ya Kitaifa inapanga upya bajeti hiyo ili kuafiki ukweli mpya. Hii itajumuisha kupunguza kwa kiasi kikubwa bajeti ili "usawa kati ya kile kinachopaswa kutekelezwa na kile kinachoweza kusubiri," na kuhakikisha kuwa programu muhimu za kitaifa haziathiriwi.

"Mpango wetu ni mzuri na thabiti na, katika utimilifu wa wakati, tutathibitishwa," Rais Ruto alisema.

Baraza la Mawaziri pia lilibainisha kuwa mashirika ya usalama yalifanya kazi nzuri ya kulinda nchi dhidi ya waliokuwa na nia mbaya.

TRT Afrika